Na MWANDISHI WETU
MKAGUZI Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Charles Kichere, amependekeza Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, iimarishe usimamizi wa ununuzi kwa kuhakikisha makadirio yanayoaminika, matumizi sahihi ya njia za ununuzi na udhibiti madhubuti wa majadiliano na mabadiliko ya mikataba ili kulinda fedha za umma.
CAG Kichere aliyasema hayo Ikulu jijini Dar es Salaam, alipowasilisha taarifa yake kwa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.
Alisema ripoti yake imebaini makadirio yasiyo sahihi ya gharama ya ujenzi wa Uwanja wa Mpira wa Miguu uliopo Arusha na pia udhaifu katika majadiliano ya zabuni ya ujenzi wa uwanja huo unaotarajiwa kutumika katika Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) mwaka 2027.
Kichere alisema kiwango cha fedha kilichotarajiwa kutumika katika ujenzi wa uwanja huo ni tofauti na kile kilichosainiwa katika mkataba wa ujenzi huo.
“Nilibaini mapungufu katika ununuzi wa mradi wa uwanja wa mpira wa Arusha wenye thamani ya sh. bilioni 338.54, hali inayoashiria kukosekana kwa thamani halisi ya fedha katika matumizi ya rasilimali za umma.
“ Kwanza, kulikuwa na tofauti kubwa kati ya makadirio na thamani ya mkataba, ambapo mradi ulikadiriwa kugharimu sh. bilioni 187, lakini ulisainiwa kwa thamani ya sh. bilioni 338.54 sawa na ongezeko la asilimia 81. Hali hii inaonyesha kuwa, makadirio hayakuwa sahihi na yaliathiri maamuzi ya kibajeti pamoja na utekelezaji wa mradi,” alisema.
Pia, CAG aliongeza kuwa: “Mkandarasi alipatikana kwa njia ya mzabuni mmoja (single source) kwa kisingizio cha dharura bila ya kuwepo ushahidi wa hali hiyo, ili kuondoa ushindani ambapo kungeweza kuhakikisha upatikanaji wa bei nafuu na kulinda maslahi ya serikali.
“Tatu, majadiliano ya zabuni yalifanyika kwa udhaifu ambapo sehemu kubwa ya vipengele vilivyojadiliwa havikuwa vimeidhinishwa kwenye mpango wa majadiliano na wigo wa kazi ulipunguzwa bila ya kupunguza gharama ipasavyo,”alisema.
Aidha, ali sema gharama zisizo halali ikiwemo sh. bilioni 3.27 za gharama za zabuni zilijumuishwa katika mkataba na kubebwa na serikali.
“Kwa ujumla mheshimiwa Rais, hali hii inaonyesha udhaifu katika upangaji wa miradi, uteuzi wa wakandarasi na usimamizi wa majadiliano ya kimkataba, udhaifu huu unaweza kusababisha matumizi yasiyo na tija na kukosekana kwa thamani halisi ya fedha za umma,” alisema.




