SELINA MATHEW NA HAMIS SHIMYE DODOMA
WAZIRI Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba, ametoa maagizo 11 kwa viongozi wa serikali na taasisi nchini kutekeleza malengo na maono ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa wananchi.
Msimamo huo aliutoa jijini Dodoma, alipowasilisha Makadirio ya Bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu, kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027, akisisitiza Rais Dk. Samia amedhamiria kuleta maendeleo kwa wananchi kwa kasi kubwa.
Dk. Mwigulu alisema Serikali imedhamiria kuleta maendeleo na kutatua kero za wanachi kwa kufanya kazi kwa bidii, weledi na ufanisi katika kutekeleza bajeti ya ofisi hiyo kwa kutoa maagizo 11 kwa viongozi.
MAAGIZO
Alitaja maagizo hayo; ni kuanza utekelezaji wa Dira 2050 kupitia mpango na bajeti ulioandaliwa kwa kuhakikisha kila sekta inasimamia rasilimali za taifa maeneo yenye tija, matokeo makubwa na kupunguza utegemezi kutoka nje.
“Lengo ni kuishirikisha sekta binafsi na wadau wa maendeleo katika kuharakisha utekelezaji wa Dira 2050 ili kujenga uchumi jumuishi, shindani na unaotegemea uzalishaji wenye tija,” alisema.
Waziri Mkuu pia aliagiza,“Wakuu wa Mikoa wanapaswa kusimamia kikamilifu maandalizi na mapokezi ya wanafunzi wa elimu ya msingi ya lazima ya miaka kumi, watakaojiunga na kidato cha kwanza mwaka 2028, kwa kukamilisha miundombinu na huduma zote muhimu.”
Aigizo la tatu, Dk. Mwigulu alitaka kuimarishwa usimamizi wa makusanyo ya mapato kwa kutumia mfumo wa kielektroniki na mashine za POS, kupunguza matumizi yasiyo ya lazima, kuziba mianya ya uvujaji wa fedha za umma na kuendeleza rasilimali fedha katika miradi ya kimkakati na kielelezo.
Dk. Mwigulu alisema agizo la nne ni wizara, taasisi na mamlaka zinazoshiriki katika uwezeshaji wananchi kiuchumi ziweke malengo yanayopimika, viashiria vya utendaji na ratiba za utekelezaji, kuhakikisha mitaji hiyo inazalisha ajira, kipato na biashara endelevu hasa kwa vijana, wanawake na wenye ulemavu.
Kwa mujibu wa Waziri Mkuu, agizo la tano ni wakandarasi wanaotekeleza miradi ya Serikali watimize wajibu wao kwa mujibu wa mikataba waliyoingia, ikiwa ni pamoja na kuwalipa watoa huduma walioshiriki katika utekelezaji wa mradi husika.
“Maofisa masuuli kuhakikisha wazabuni na watoa huduma wanalipwa kwa wakati kwa mujibu wa makubaliano na huduma iliyotolewa,”alisema.
Agizo la sita, Waziri Mkuu aliwataka wakuu wa mikoa kuhakikisha ndani ya miezi sita baada ya kuanza utekelezaji wa Bajeti ya Mwaka 2026/2027, wahakikishe shule zote katika halmashauri zina matundu ya vyoo kwa kuzingatia uwiano wa wanafunzi waliopo.
“Agizo la saba ni Wizara ya Maji; ihakikishe huduma ya maji inapatikana katika shule na vituo vyote vya kutolea huduma ya afya ndani ya miezi sita baada ya kuanza utekelezaji wa bajeti ya mwaka 2026/2027. Baada ya muda huo, ni marufuku kwa wanafunzi kubeba maji na kupeleka shuleni,” alisema.
Waziri Mkuu Dk. Nchemba alisema agizo la nane ni ubora wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika sekta mbalimbali nchini, iwiane na thamani ya fedha iliyotolewa.
Alisisitiza; “Fedha zinazoelekezwa na Serikali kwenye miradi hiyo zitumike kama ilivyokusudiwa. Vilevile, wakandarasi wa ndani wawe wazalendo kwa kutumia ipasavyo fursa inayotolewa ya ushiriki wa kampuni zilizosajiliwa ndani kutekeleza miradi mikubwa.”
Waziri Mkuu alisema agizo la tisa; wizara za kisekta, taasisi na Mamlaka za Serikali za Mitaa zilipe fidia kwa wananchi wanaopisha maeneo ya utekelezaji wa miradi ya Serikali kabla ya kutwaliwa kwa maeneo yao kwa kuzingatia taratibu zilizopo.
“Taasisi zote za umma ziimarishe ufuatiliaji na tathmini ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali za Serikali ikiwemo mipango, programu na miradi kuongeza tija ya utendaji kazi na kuboresha huduma kwa wananchi,” alisema.
Kwa upande wa agizo la 11, alizitaka wizara, mikoa, Mamlaka za Serikali za Mitaa, taasisi, wakala na idara zinazojitegemea kuanza kutekeleza mapendekezo ya Tume ya Rais ya Kutathmini Maboresho ya Mfumo wa Kodi kama alivyoelekeza Rais.
AOMBA TRILIONI 12.5
Waziri Mkuu aliomba kuidhinishiwa jumla ya Sh trilioni 12.5, kwa ajili ya Ofisi yake na taasisi zilizo chini yake kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027, zikilenga kuimarisha uchumi na utoaji wa huduma kwa wananchi.
Dk. Mwigulu alisema kati ya fedha hizo sh. trilioni 8.73 ni za matumizi ya kawaida, huku sh. trilioni 3.76 zikielekezwa katika miradi ya maendeleo.
Alisema pia, Serikali imeomba sh. bilioni 225.02 za Mfuko wa Bunge, kati ya hizo sh. bilioni 207.99 ni kwa matumizi ya kawaida na sh. bilioni 17.02 maendeleo.
Pia, alisema katika Mwaka wa Fedha 2026/27 ofisi hiyo inatarajiwa kukusanya maduhuli na mapato ya ndani ya jumla ya sh. trilioni 2.4.




