Na REHEMA MOHAMED
WAZIRI Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba, ameagiza hatua za haraka zichukuliwe kurejesha biashara katika Soko la Mawasiliano Simu 2000, Sinza, Wilaya ya Ubungo jijini Dar es Salaam.
Dk. Mwigulu aliyasema hayo, alipokagua madhara ya tukio la moto lililotokea Aprili 4, 2026, ambalo takriban vibanda 500 vya wafanyabiashara wadogo viliteketea.
Akizungumza na wafanyabiashara hao, Waziri Mkuu alisema serikali inaendelea kufuatilia kwa karibu tukio hilo, na itatoa kauli rasmi baada ya kukamilika uchunguzi wa kina ulioelekezwa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.
“Rais amepata taarifa ya jambo hili, anawapa pole sana na ameelekeza uchunguzi wa kina ufanyike ili tujue chanzo cha tatizo hili. Na kazi hiyo imeanza ili tuweze kupata undani wa chanzo cha jambo hili lililojitokeza,” alisema.
Aidha, Waziri Mkuu aliagiza eneo la soko hilo kusafishwa mara moja kuruhusu wafanyabiashara kuanza taratibu za kurejesha shughuli zao.
“Mkurugenzi, ukitoka hapa leo (jana) wakati unamalizia siku…, kesho hapa pote pasafishwe. Hii kazi ya kusafisha kesho iishe,” aliagiza Waziri Mkuu.
Alisema serikali itashirikiana na taasisi za kifedha kusaidia wafanyabiashara wenye mikopo waliopoteza mitaji yao, kuweka utaratibu wa kuwaongezea muda wa kurejesha mikopo hiyo na kuwezesha upatikanaji mikopo mipya yenye nafuu kupitia mamlaka za serikali za mitaa.
“Mkurugenzi sasa kwenye mikopo mipya nenda kaangalie una ukoko gani… tufanye kipaumbele kwa hawa ambao mtaji wao umeungua ili wapate haraka,” alisema.
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu aliagiza kuwepo eneo la stendi katika mpango wa ujenzi wa soko hilo, kurahisisha shughuli za biashara.
Dk. Mwigulu alikemea vitendo vya ulanguzi wa vibanda katika masoko na kusisitiza vibanda vitolewe kwa wafanyabiashara halisi wanaofanya biashara.
AMANI YA NCHI
Vilevile, aliwataka wananchi kushirikiana katika kulinda amani na utulivu wa nchi, akisisitiza amani ni msingi wa shughuli zote za kiuchumi.
“Ni lazima tuwe na amani kwenye nchi yetu. Kila Mtanzania awe mdau wa amani katika nchi yetu,” alisema.
Kwa upande mwingine, Waziri Mkuu alisisitiza umuhimu wa kuheshimu sekta binafsi katika kukuza uchumi wa nchi, akieleza ndiyo mhimili mkuu wa ajira kwa Watanzania.
PROFESA KITILA
Mbunge wa Jimbo la Ubungo, ambaye ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo, alisema uchumi wa wilaya hiyo unategemea masoko manane.
Profesa Kitila, alimwomba Waziri Mkuu kujengewa stendi ya mabasi kurahisisha utendaji kwa wafanyabiashara wa Soko la Simu 2000.
KATAMBI
Kwa upande wa Waziri wa Mambo ya Ndani, Patrobas Katambi, alidokeza kupititia janga hilo, wamejifunza na wamejipanga kukabiliana na majanga ya moto.
“Maeneo mengi kama ya masoko yakitokea majanga ya moto mfano Soko la Kariakoo, lilichagizwa kwa kuwekewa vifaa vya kukabiliana na moto yakiwemo magari 140.
“Pia, vifaa vya kisasa vya kuzima moto na kuboresha mafunzo kuhakikisha katika kila maeneo wanaweka vyombo vya kuzimia moto kwa ukaribu,” alisema.
Waziri huyo alitoa wito kwa wananchi kuendelea kutoa taarifa mapema yanapotokea majanga ya moto, ili kazi ya uokoaji ifanyike kwa ufanisi.
Katambi alisema wizara itaendelea kutoa elimu katika masoko na maeneo mengine ya wananchi kukabiliana na majanga ya moto.
DC UBUNGO
Mkuu wa Wilaya ya Ubungo, Albet Msando, aliiomba serikali kuweka mazingira haraka ya usafi wafanyabiashara hao warejee kazini.
Msando alisema endapo wafanyabiashara hao wataendelea kubaki nyumbani, idadi kubwa watapata changamoto ya maisha.
Pia, Msando aliomba wafanyabiashara hao wapatiwe mikopo haraka waanze kufanya biashara, baada ya kupoteza mitaji yao katika ajali hiyo.
WAFANYABIASHARA
Mfanyabiashara Samaduu Bakari aliomba kamati iliyochaguliwa kwa uboreshaji wa soko hilo, iondoke na wachaguliwe viongozi wengine.
“Mwenyekiti aliyetajwa kwa jina la Musendile ana watu wake wa chini, uongozi wake si mzuri kwa sababu wanagawa maeneo na baadhi wanajigawia.
“Kamati ilichakachuliwa mara tatu, hatutaki mtu anayechukua fursa kuwaumiza wengine, hiki kitu kimetokea, umeagiza hapa pasafishwe, lakini kesho ukija utaambiwa hili eneo la mtu fulani limepangishwa, hiki ninachoongea ni cha kweli kabisa,” alisema.
Mkuu wa Wilaya ya Ubungo, Albet Msando akijibu hoja hiyo, alisema baadhi ya watu walikuwa wakitumia siasa kujinufaisha kupitia wafanyabiashara.
Aliwaahidi wafanyabiashara atasimamia suala hilo kwa kujua nani anaingia nani anatoka na anakotokea.
Msando alisema kamati ya usalama ya wilaya itashinda hapo na aliahidi kujenga ofisi ya muda hapo huku kamati husika ikichaguliwa kwa uwazi na vijana wa kulinda eneo hilo watachaguliwa.
Mfanyabiashara Tisamo Kibule, aliomba mitaji ya mikopo ipatikane haraka na ujenzi wa soko uanze haraka.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Ubungo, Aron Kagurumjuli, alisema wana sh. bilioni mbili ambazo Waziri Mkuu aliagiza ndani ya wiki mbili wafanyabiashara waliounguliwa wakopeshwe wapate mitaji.
“Mstahiki Meya na Mkuu wa Wilaya mtajua cha kufanya tuwarudishe watu kazini, mtaliangalia hilo mpate cha kuanzia watu waendelee na kazi,” aliagiza Waziri Mkuu.
Kwa Charles Godlack aliomba mikopo itakayotolewa iwe na masharti nafuu na pia wapewe muda wa kufanya biashara kabla ya kuanza kulipa.




