Dodoma
NA SELINA MATHEW
RAIS DK. Samia Suluhu Hassan, ameendelea kuwa mstari wa mbele kutatua tatizo la ajira kwa vijana nchini, baada ya kuja na mpango wa kuwawezesha kiuchumi kupitia mikopo yenye masharti nafuu.
Mpango huo, unatarajiwa kuwasilisha Bungeni na serikali kupitia muswada wa mabadiliko ya sheria za dhamana za mikopo, hatua inayolenga kuruhusu matumizi ya mali zinazohamishika ikiwa ni dhamana rasmi katika utoaji wa mikopo.
Mapendekezo hayo yanakuja katika wakati ambapo kundi kubwa la vijana na wajasiriamali wadogo wamekuwa katika changamoto ya fursa za kifedha kutokana na ukosefu wa dhamana za jadi kama nyumba na ardhi.
Ikiwa muswada huo utapitishwa kuwa sheria, utafungua ukurasa mpya kwa sekta ya fedha kuruhusu matumizi ya mali kama vifaa vya biashara, mashine na rasilimali nyingine zinazohamishika kupata mikopo.
Akizungumza mjini Dodoma, Waziri Mkuu Dk. Mwigulu Nchemba, alisema sh. bilioni 280 zimetengwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), kutumika kama dhamana kwa vijana, ikiwa ni sehemu ya mpango wa vijana kukopesheka kupitia vyeti vya kuhitimu, kuwawezesha kujiajiri na kukuza uchumi.
Dk. Mwigulu aliyasema hayo wakati akijibu swali la papo kwa hapo la Mbunge wa Viti Maalumu, Timida Fyandomo.
Katika swali lake, Mbunge huyo alisema kwa mujibu wa takwimu mbalimbali za kitaifa kati ya vijana 600,000 hadi milioni moja wanaingia katika soko la ajira kila mwaka, huku zinazozalishwa zikiwa hazina uwiano mkubwa.
Alihoji, serikali ina mkakati gani wa kuwawezesha vijana kuwekeza na kuwaunganisha na wawekezaji mbalimbali ndani na nje ya nchi, kukuza wigo wa ajira.
Akijibu swali hilo, Dk. Mwigulu alibainisha kuwa suala hilo lipo katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), kutengeneza ajira zipatazo milioni nane na mikakati ya utekelezaji wa mipango ya maendeleo ya nchi iliyopo katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
“Pato tunaloongelea la takribani dola trilioni moja ifikapo 2050, tunatarajia mchango mkubwa utoke kwa vijana, tunaandaa mazingira bora ambayo yatawawezesha kupata ajira ndani ya sekta ya umma na binafsi,” alisema.
Alisema tayari imeshapitishwa sheria ya uwekezaji ya 2025, ambapo vijana watanufaika na vivutio ambavyo wanapata wawekezaji wakubwa.
“Tumeweka vijana wa hapa wakishapata cheti cha TISEZA wanaweza kunufaika na vile vivutio ambavyo wawekezaji wakubwa walikuwa wanapata ikiwemo Ardhi, mapunguzo katika kodi, ushuru, tozo mbalimbali.
Aliongeza: “Kwenye yale madirisha ambayo wawekezaji wakubwa walikuwa wanapata, sasa tumefungua vijana wanaweza kupata fursa hizo ikiwemo la kuwanufaisha na viwanda, masoko, kuwaunganisha na taasisi za kifedha jambo lililokuwa linakwamisha vijana wetu.”
Aidha, alisema Rais Dk. Samia ameunda Wizara mpya inayohusika na masuala ya vijana, lengo ni kuhakikisha wananufaika na fursa zinazojitokeza ikiwemo ufunguzi wa dirisha la kutoa dhamana kwa vijana, ambalo ndani ya mwaka huu linatarajiwa lianze kutumika.
“Hii itakuwa kampuni ya kutoa dhamana kwa vijana ambapo vijana wengi watanufaika zaidi, tayari ndani ya Benki Kuu ya Tanzania kuna shilingi bilioni 280 zimewekwa kwa ajili ya kutumika kama dhamana kwa vijana,” alisema.
Alibainisha kuwa wameanza kuwaza kwamba kijana aweze kutumia cheti chake kile alichohitimu kukopa, kama atamaliza famasia na inajulikana hivyo atumie cheti kukopa aanzishe famasi, kama uhandisi akope.”
Alisisitiza kuwa watakapomaliza kutengeneza sheria jambo hilo litaletwa bungeni kuwezesha kutengeneza kampuni ya kutoa dhamana na kuweka dhamana mali ambazo zinazoweza kuhamishika.
Aidha, alisema ajenda hiyo ni ya kidunia huku akieleza ni ukweli kwamba vijana wengi wanaingia katika soko la ajira, ambapo zamani ilikuwa wakiwa bado masomoni walikuwa wanapokea barua za kuambiwa wachague kazi wanazotaka kwenda kufanya zaidi ya moja.
“Kwa sasa siyo jambo la ajabu kukuta mstaafu yupo na wasomi wawili wakiwa tegemezi kwake, hivyo ni jambo na ajenda kubwa ambayo mbunge ameleta,” alisema.




