Na ATHNATH MKIRAMWENI
BAADHI ya wadau wa elimu nchini, wamesema wanatarajia mchakato wa Tume ya kuchunguza matukio ya uvunjifu wa amani wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu, Oktoba 29, mwaka jana, unaoendelea utaleta matokeo chanya yatakayosaidia kuimarisha demokrasia na kudumisha umoja wa kitaifa.
Pia, kuendeleza amani nchini na utekelezaji wa falsafa ya 4R ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.
Akizungumza na UHURU, Mhadhiri Mwandamizi kutoka Chuo cha Mwalimu Nyerere, Dk. Philip Daninga, alisema hatua ya kuipa tume muda zaidi ni ya hekima kwani itaiwezesha kupokea na kuchakata taarifa za ziada kwa kina, hali itakayosaidia kupatikana kwa taarifa sahihi na yenye manufaa kwa taifa.
Alieleza kuwa taarifa hiyo itakuwa nyenzo muhimu kwa Rais Dk. Samia katika kuendeleza misingi ya maridhiano, ustahimilivu, mageuzi na kujenga upya taifa, huku ikichangia kuimarisha utulivu na mshikamano wa Watanzania.
Pia, alisema matarajio ni kuona tume hiyo ikiweka mazingira bora ya ushiriki wa wananchi katika mchakato wa uchaguzi kwa kuhakikisha unakuwa huru, wa haki na shirikishi, kuondoa changamoto zilizojitokeza hapo awali.
Dk. Daninga alisisitiza umuhimu wa kujifunza kutokana na yaliyopita ili kuimarisha demokrasia na kujenga uelewa mpana wa wananchi kuhusu haki zao za kiraia na wajibu wao katika kulinda amani ya nchi.
Aliongeza kuwa taasisi za elimu zina jukumu kubwa la kusambaza maarifa hayo kwa jamii, hasa kwa vizazi vya sasa na vijavyo, kujenga utamaduni wa kuheshimu demokrasia, kushiriki uchaguzi kwa uwajibikaji na kuthamini amani kama tunu ya taifa.
Alitoa wito kwa Watanzania kutumia siku 21 zilizotolewa kutoa maoni yao kwa utulivu na bila vitisho, akisisitiza umuhimu wa kuendeleza umoja, uzalendo na mshikamano wa kitaifa kwa maendeleo ya nchi.
Mhadhiri Mwandamizi kutoka Chuo Kikuu Huria Tanzania(OUT) Mohamed Maguo aliwataka Watanzania kuwa na subira na kuendelea kuwa na imani na tume hiyo.
Alisema anaamini tume hiyo itakuja na taarifa nzuri itakayoimarisha umoja na amani ya taifa.
“Ni hatua nzuri tume kuongezewa muda, hiyo itachochea kuja na kukamilisha vizuri kazi iliyosalia na taarifa watakayoitoa itasheheni mambo yatakayokuwa na majibu kitaalamu.
“Sasa kupata suluhisho la tatizo ni lazima kufanya utafiti, kuongezewa muda ni kitu kizuri kwa sababu wanalo lengo la kila kitu watakachokileta kitakuwa sahihi kwa mujibu wa utaalamu unaotakiwa, hivyo hatua zitakazochukuliwa zitakuwa sahihi kumaliza tatizo lisije jirudia,”alisema.
Kwa upande wake, Mhadhiri kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma, Dk. Luka Mkonongwa, alisema wanatarajia tume itakuja na taarifa itakayokidhi kiu ya Watanzania, hivyo aliwataka wananchi kuwa na subira.
Alisema wanatarajia matokeo yatakayokuja kutolewa yatakuwa na mchango mkubwa katika kuboresha sera na mifumo ya uchaguzi.
“Ninategemea tutapokea matokeo chanya yatakayotupeleka katika hali bora zaidi ya namna ya kuendesha uchaguzi wetu,” alisema.
Maoni ya wadau hao yamekuja baada ya Tume hiyo kuongezewa muda wa siku 21, kukamilisha kazi yake na hatua hiyo imetokana na tume kushindwa kumaliza majukumu ndani ya muda wa nyongeza ya awali.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mwenyekiti wa tume hiyo, Jaji Mkuu mstaafu wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Othman Chande, baada ya muda wa awali, wananchi waliendelea kujitokeza kwa wingi tofauti na matarajio ya tume, hivyo kuongeza idadi ya ushahidi, taarifa na maoni yaliyopokelewa.
Alisema hali hiyo ilisababisha tume kushindwa kukamilisha kazi ndani ya muda uliotolewa.
Tume hiyo ilianza kutekeleza majukumu yake Novemba 20, mwaka jana, ikiwa na matarajio ya kukamilisha kazi ndani ya siku 90, lakini kutokana na sababu mbalimbali, iliongezewa muda na kutakiwa kuwasilisha ripoti kwa Rais kabla au ifikapo Aprili 3, mwaka huu.
“Kutokana na hali hiyo, tume iliomba muda wa ziada kukamilisha majukumu yake, ambapo mamlaka ya uteuzi imeridhia ombi hilo na kuongeza muda wa siku 21, huku ikiitaka tume kukamilisha kazi kabla au ifikapo Aprili 24, mwaka huu,” ilisema taarifa hiyo.
Ilitaja sababu za kuongeza muda ni kuwezesha uchambuzi wa ushahidi, taarifa na maoni yaliyopokelewa, kutoa nafasi kwa wataalamu wa uchunguzi wa kisayansi kufanyia kazi vielelezo vipya, kukamilisha maandalizi ya ripoti itakayowasilishwa kwa rais na kuandaa tafsiri ya ripoti hiyo.
Tume hiyo iliwashukuru wananchi na wadau kwa ushirikiano walioutoa katika kipindi cha uchunguzi, wakiwemo waliofika kutoa ushahidi, waliopiga simu, kutuma ujumbe, kuwasilisha maoni kwa maandishi na kupitia mitandao ya kijamii.
Novemba 20, mwaka jana, Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, aliizindua tume hiyo na kuipa siku 90 za kufanya uchunguzi huo hadi Februari 20, mwaka huu.
Februari 21, mwaka huu, tume hiyo iliongezewa muda wa siku 42, huku taarifa ya uchunguzi ikitarajiwa kuwasilishwa Aprili 3, mwaka huu.




