Na MWANDISHI WETU
RAIS wa klabu ya Yanga Injinia Hersi Said, ameweka wazi kuhusu sakata la usajili wa kiungo wao Mohamed Damaro, akisisitiza kuwa mchezaji huyo ni Mtanzania.
Akizungumza na Shirika La Utangazaji Tanzania (TBC),Dar es Salaam, Hersi alisema leseni ya Damaro pamoja na mfumo wa usajili wa FIFA (TMS) vinamtambua kama Mtanzania.
Alifafanua usajili wa mchezaji huyo, upo sahihi na hakuna kitu kilicho tofauti na kanuni.
“Leseni ya Damaro inasoma kama mchezaji mtanzania tangu Januari 2025, sisi tukimtazama katika mfumo ambao FIFA wanautambua (TMS) mfumo unamtambua kama mchezaji wa Kitanzania, kwa hiyo sisi kama Yanga ukituingiza katika hilo sakata unatukosea.” alisema Hersi.
Alisema mfumo wa ‘Transfer Matching System’ ni Uhamisho unaolingana na mfumo maarufu TMS ambao unamtambua Damaro kama mchezaji wa Tanzania na si raia wa Guinea.
Alisema Damaro alijiunga na Yanga, awali alikuwa anaichezea timu ya Singida Black Stars kama mchezaji wa ndani.
“Madai yanayoikosoa Yanga kuvunja taratibu za usajili hayana msingi na yanapotosha ukweli,”alisema kiongozi huyo.
Kauli hiyo, imekuja baada ya hivi karibuni Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Simba Crescentius Magori alidai kuwa wameomba kuhakiki ‘review’ kwa TFF kuhusu sakata hilo.
Alisema baada ya hapo watasonga mbele katika Mahakama ya Usuluhishi ya Michezo(CAS) na Shirikisho la Soka la Kimataifa ( FIFA).
Pia, kiongozi huyo alisema ujenzi wa uwanja, wamefikia hatua nzuri ya mchakato.
“Katika ujenzi wa uwanja tumefika kwenye eneo zuri sana. Tunafanya mchakato wetu kwa umakini mkubwa na kwa usahihi. Tuliwatangaza GSM kuwa washindi wa tenda ya ujenzi wa uwanja. Tayari tumepata mchoro wa awali wa uwanja,”alisema.
Aliongeza kuwa klabu imeshatoa maoni kuhusu mchoro huo na jana wamekamilisha michoro yote na gharama za ujenzi zote.
Kiongozi huyo alisema klabu Yanga ina wajibu wa kukuza lugha ya Kiswahili katika mchezo wa soka hapa nchini na nje ya nchi.
“Mimi na Rais wa Shirikisho la Mpira Tanzania, Wallace Karia, tunao wajibu mkubwa wa kuhakikisha lugha ya kiswahili inapenya kwa kiwango kikubwa katika medani za kimichezo za kimataifa Hususan CAF.
“Tukiwa na mshikamano madhubuti tutafanikisha lengo hili la kuweka lugha yetu hii katika daraja ambalo inastahili,” alisema Mhandisi Hersi Said.




