Na ZIANA BAKARI
WACHUMI nchini, wamewataka Watanzania kuendelea kumuunga mkono Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, katika jitihada zake za kuimarisha ustawi wa taifa.
Pia, wamesisitiza umuhimu wa kudumisha amani, umoja na mshikamano ikiwa ni msingi imara wa maendeleo endelevu ya taifa, wakieleza kuwa misingi hiyo ni chachu ya kuleta mafanikio ya nchi.
Wasomi na wachumi hao, walitoa kauli hiyo kwa nyakati tofauti jana, walipozungumza na gazeti hili, huku wakimpongeza Rais Samia kwa kutunukiwa Shahada ya Heshima ya Udaktari wa Fasihi na Chuo Kikuu cha Jimbo la Nasarawa cha Nigeria ambayo ni heshima kwake na Tanzania.
DK. MAGUO
Mhandhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT), Dk. Mohamed Maguo, alisema shahada hiyo aliyopewa, inatoa taswira kuwa, Rais Dk. Samia, anafanya kazi kwa bidii na kujituma katika majukumu yake ya uongozi.
Alisema hatua hiyo ni uthibitisho wa mchango wake mkubwa katika kuimarisha maendeleo ya taifa na kuzidi kuitangaza nchi kimataifa zaidi.
“Ni heshima kubwa kiongozi wetu kutambulika nje ya nchi kutokana na juhudi zake. Ni heshima kwa Watanzania.
“Tunachopaswa kufanya Watanzania ni kuendelea kumuunga mkono Rais Dk. Samia kwa kufanya kazi kwa bidii.
“Tujitahidi kuendelea kudumisha amani, umoja na mshikamano kama msingi imara wa maendeleo endelevu ya taifa, Rais Dk. Samia, azidi kufanya vizuri maendeleo ya nchi yaweze kuonekana zaidi nje,” alisema.
DK. TIMOTHY LYANGA
Mhadhiri wa Uchumi wa Chuo cha OUT, Dk. Timothy Lyanga, alimpongeza Rais Samia kwa kutunukiwa shahada hiyo, ambayo inaakisi jitihada zake anazofanya katika uongozi wake.
Alisema ni ishara ya kutambuliwa kwa mchango wake katika kuimarisha maendeleo ya taifa na kukuza heshima ya Tanzania kimataifa.
“Shahada hiyo aliyopewa Rais Samia, inasaidia kuimarisha uhusiano mzuri kati ya nchi hizo, jambo ambalo ni muhimu kwa Watanzania ni kuendelea kuiunga mkono serikali kwa kila jitihada inazozifanya,”alisema.
Dk. Lyanga, alisema uhusiano huo mzuri, utachochea ushirikiano wa kiuchumi, kisiasa na kijamii na kufungua fursa zaidi ambazo zitachochea maendeleo ya pamoja kati ya nchi hizo mbili.
DK. PHILIP DANINGA
Mhadhiri Mwandamizi wa Uchumi na Uongozi wa Chuo cha Mwalimu Nyerere (MNMA), Dk. Philip Daninga, alisema Rais Samia, anaendelea kudhihirisha kuwa, uongozi wake ni imara, wenye maono na unaozingatia matokeo chanya kwa maendeleo ya taifa.
Alieleza kuwa, uimara huo wa uongozi umechangia kutunukiwa shahada hiyo ambayo imeakisi jitihada zinazofanywa na Watanzania kwa ushirikiano wenye utu katika kujenga taifa.
“Shahaha hiyo siyo tu heshima kwa kiongozi, bali ni kielelezo cha mshikamano na bidii ya Watanzania katika kushiriki maendeleo ya nchi yao.
“Mafanikio haya yanatakiwa kuwa chachu ya kuongeza bidiii kwetu kuimarisha umoja na kudumisha amani ili taifa liendelee kupiga hatua zaidi katika nyanja zote za maendeleo,”alisema.
Juzi, Rais Dk. Samia alitunukiwa shahada hiyo katika Sherehe ya Mahafali ya Nane ya chuo hicho iliyofanyika katika Kampasi Kuu ya Keffi, nchini humo, huku akishiriki kwa njia ya mtandao akiwa Ikulu Chamwino, Dodoma. akisema ni heshima kubwa kwake na Tanzania.
Alisema aliipokea kwa heshima na unyenyekevu mkubwa na inaakisi jitihada zinazofanywa na Watanzania kwa ushirikiano wenye utu katika kulijenga taifa.
Chuo hicho, kilimtunuku shahada hiyo, Rais Samia kwa kutambua uongozi wake wa kuwa kinara wa nishati safi ya kupikia, kuimarisha afya ya mama na mtoto, taswira nzuri katika masuala ya uongozi kwa wanawake Afrika na Kusimamia masuala ya biashara hususani kwa vijana Afrika.
Rais Dk. Samia, alisema alipokea heshima hiyo kwa unyenyekevu, akieleza mafanikio hayo yanaakisi juhudi za pamoja za Watanzania kuendeleza maendeleo na ushirikiano wa Bara la Afrika.
“Napokea heshima hii kwa unyenyekevu mkubwa. Tuzo hii siyo yangu pekee, bali inaakisi jitihada za pamoja za wananchi wa Tanzania katika kuendeleza maendeleo, ushirikiano na ustawi wa Bara la Afrika,” alisema Rais Samia.
Aidha, akirejea safari yake ya uongozi, Rais Samia alisema uzoefu wake hadi kufikia nafasi ya juu ya uongozi wa kitaifa, unatoa chachu ya kuendelea kufungua fursa na kuondoa vikwazo vinavyokwamisha wanawake, vijana kushiriki kikamilifu katika uongozi na uamuzi wa maendeleo barani humo.




