Na LILIAN JOEL, Arusha
WAZIRI Mkuu Dk. Mwigulu Nchemba, ameagiza Mamlaka ya Serikali za Mitaa, kubuni vyanzo vipya vya mapato.
Pia, ameagiza kudhibiti upotevu wa mapato ili kurahisisha utekelezaji wa elimu ya lazima ya miaka 10, Bima ya Afya kwa Wote na Dira ya Taifa ya Maendeleo ya Taifa ya Mwaka 2050, ambayo moja ya malengo yake ni kuwa na pato la taifa la sh. trilioni moja kwa mwaka.
Aidha, Waziri Mkuu alitoa mchango wa sh. milioni 50 kusaidia kununua gari kwa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT), anayemaliza muda, Mirshid Ngeze, ambaye amepata ulemavu wa kudumu akiwa kazini.
Dk. Mwigulu alisema hayo jijini Arusha, akifungua mkutano wa mkuu maalumu wa uchaguzi wa viongozi wa ALAT.
“Ndani ya mwaka mmoja ujao, tunakwenda kufanya mabadiliko makubwa ya kuwa na elimu ya lazima ya miaka 10 na nyie ndiyo mtakaobeba mzigo huo.
“Watoto zaidi ya milioni tatu kwa mwaka 2028, watajiunga na kidato cha kwanza na tutahitaji vyumba vya madarasa zaidi ya 23,000 na vyumba vya maabara zaidi ya 9,000 ambapo miundombinu hiyo itagharimu zaidi ya shilingi bilioni moja,”alisema Waziri Mkuu.
Aliitaka ALAT kujenga uhusiano mzuri kwa kuziimarisha sekta binafsi, zitoe mchango wa utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Mwaka 2050 kwa asilimia 70.
Alisema Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, anatambua kazi kubwa inayofanywa na ALAT, hivyo aliwataka kutembea kifua mbele kwa kuwa, miradi ya serikali inatekelezwa kwa kiwango.
“Ninyi ni mashahidi wa miradi hii na ulinganisho huo wa takwimu za miradi katika kipindi cha uongozi wa Rais Dk. Samia wa miaka minne, ambacho kimeleta tabasamu kwa Watanzania.
“Ndani ya miaka minne, Rais Samia alitoa fedha za ujenzi wa vyumba vya madarasa zaidi ya 79,000, shule za msingi 2,700, shule za sekondari 1,300 na shule za amali 103.
Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Profesa Riziki Shemdoe, alimshukuru Rais Samia kuridhia fedha nyingi zielekezwe Mamlaka za Serikali za Mitaa kutekeleza miradi ya maendeleo.
“Tutahakikisha tunaipeleka nchi katika sehemu salama ambayo italeta tabasamu kwa wananchi, kutokana na kazi kubwa inayofanywa na wakurugenzi wa halmashauri nchini,” alisema Profesa Shemdoe.
Awali, Mwenyekiti wa ALAT anayemaliza muda wake, Ngeze alisema ameacha mchakato wa ujenzi wa jengo la Makao Makuu ya ALAT jijini Dodoma.
“Tunaiomba serikali mtusaidie kuboresha maslahi ya madiwani wa halmashauri nchini na kutoa vibali vya madiwani kufanya mafunzo nje ya nchi, kujifunza utawala bora na ukusanyaji mzuri wa mifumo ya mapato,” alisema.




