Na MUSSA YUSUPH, Dodoma
SERIKALI imetoa wito kwa wananchi kujitokeza katika vituo vya kutoa huduma za afya kupima magonjwa ya afya ya akili hususan msongo wa mawazo na sonona, baada ya kubainika ongezeko kubwa la wagonjwa hayo yanayochangiwa na changamoto mbalimbali za kijamii.
Takwimu kutoka Wizara ya Afya, zimeonesha kuwa, kipindi cha Julai mwaka jana hadi Machi mwaka huu, wananchi 1,709 wamepimwa huku 1,362, wamegundulika kuwa na matatizo hayo ya afya ya akili
Pia, takwimu hizo zimebainisha kuwa, magonjwa ya mfumo wa hewa, maambukizi ya njia ya mkojo (UTI), malaria na kuharisha, yanaongoza kwa idadi ya wagonjwa waliofika hospitalini kupatiwa matibabu kwa mwaka wa fedha 2025/2026.
Akiwasilisha hotuba ya makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 bungeni jijini hapa juzi, Waziri wa Afya, Mohammed Mchengerwa, alisema upatikanaji dawa za afya ya akili katika vituo, umefikia wastani wa asilimia 75.
“Huduma za afya ya akili na msaada wa kisaikolojia, ziliendelea kutolewa katika vituo vya kutolea huduma za afya ngazi ya msingi nchini, ambapo wateja 254,932, walihudumiwa katika kipindi cha Julai mwaka jana hadi Machi mwaka huu.
Alieleza: “Huduma hizo, zilijumuisha matibabu ya kifafa, skizofrenia, matatizo ya tabia, utegemezi wa pombe na dawa za kulevya.”
Mchengerwa alibainisha kuwa, hadi sasa, vituo 16 vya matibabu ya waraibu wa dawa za kulevya, vilitoa huduma kwa wateja 17,807 huku upatikanaji dawa za afya ya akili katika vituo, umefikia wastani wa asilimia 75.
Vilevile, alisema mafunzo kwa wataalamu wa afya ngazi ya jamii yakihusisha wahudumu wa afya ngazi ya jamii 50 na wahudumu wa afya 10.
Alisema lengo ni kuwawezesha kutambua na kutoa huduma kwa watu wenye changamoto za msongo wa mawazo na sonona katika jamii husika ambapo kwa kipindi cha Julai mwaka jana hadi Machi mwaka huu, wanajamii 1,709 wamepimwa na 1,362 wamegundulika kuwa na sonona, wapo kwenye tiba.
Pia, alisema elimu kuhusu ugonjwa wa kifafa ilitolewa kwa jamii kupitia maadhimisho ya Siku ya kifafa Duniani pamoja mikutano.
“Nitoe rai kwa wananchi wote, kujitokeza kwa wingi kwenda katika vituo vya kutolea huduma za afya kupima magonjwa ya afya ya akili hususan hali ya msongo wa mawazo na sonona inayoonekana kuongezeka ili kuepusha madhara zaidi, kwani hali hii inatibika,” alisisitiza.
MAAMBUKUZI YA HEWA, UTI NA MALARIA YAONGOZA
Katika hatua nyingine, Mchengerwa alieleza kuwa, watu milioni 39.9, walipata huduma za matibabu nchini katika mwaka wa fedha 2025/2026, huku magonjwa ya mfumo wa hewa, maambukizi ya njia ya mkojo (UTI), malaria na kuharisha yakiongoza kwa idadi ya wagonjwa waliofika hospitalini.
Mbali na magonjwa hayo, alisema maradhi ya ngozi, shinikizo la damu na magonjwa yasiyoambukiza (NCDs), nayo yameendelea kuwa changamoto kwa wananchi.
Katika kuimarisha huduma za afya, alisema serikali imeendelea kukuza tiba asili ambapo dawa 48, zimesajiliwa huku dawa sita zikipelekwa katika tafiti za usalama na dawa mbili za kisukari zikifanyiwa utafiti wa ufanisi. Wagonjwa 648, wamehudumiwa kupitia hospitali jumuishi zinazotoa tiba asili na tiba za kawaida.
Akichangia mjadala huo, JOHANNES LUKUMAY Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na Masuala ya Ukimwi, Johannes Lukumay, aliipongeza serikali kuimarisha huduma za afya hususan uchunguzi wa magonjwa kupitia ongezeko kubwa la vifaa vya kisasa vya tiba.
Alisema serikali imenunua na kusimika vifaa vya uchunguzi, matibabu na huduma za ubingwa vyenye thamani ya sh. bilioni 241.6 katika kipindi cha mwaka 2021 hadi 2026.
Alieleza kuwa, hatua hiyo imeongeza uwezo wa hospitali nyingi nchini kufanya uchunguzi wa magonjwa kwa haraka na usahihi zaidi ambapo mashine za MRI zimeongezeka kutoka saba hadi 13, CT Scan kutoka 12 hadi 45 na Digital X-ray kutoka 147 hadi 559.
Lukumay alisema vifaa vya Ultrasound vimeongezeka kutoka 476 hadi 970 huku Serikali pia ikiongeza huduma za kibingwa kama upandikizaji figo, upasuaji wa ubongo, kuzibua mishipa ya moyo na huduma za saratani kwa teknolojia ya PET-CT.




