Na MWANDISHI WETU
TANZANIA na Kenya zimekubaliana kuharakisha utekelezaji wa miradi mbalimbali ya njia za umeme zinazounganisha gridi za nchi hizo pamoja na kuboresha mifumo ya usafirishaji wa umeme.
Lengo la hatua hiyo ni kuimarisha usalama wa nishati, kuongeza uhakika wa upatikanaji wake na kukuza biashara ya umeme Afrika Mashariki.
Makubaliano hayo yalifikiwa baada ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Felchesmi Mramba, kufanya mazungumzo na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Mafuta wa Kenya, Alex Wachira, jijini Nairobi, Kenya, leo Mei 14, 2024.
Mazungumzo hayo yalijikita kuimarisha ushirikiano katika sekta ndogo ya umeme na nishati jadidifu, hususani biashara ya umeme, utekelezaji wa miradi ya uunganishaji wa gridi na kuboresha mifumo ya usafirishaji na usambazaji umeme kati ya nchi hizo.
Viongozi hao pia walijadili hatua mbalimbali za kuimarisha biashara ya umeme katika ukanda wa Afrika Mashariki kupitia Umoja wa Soko la pamoja la Kuuziana Umeme na Kuimarisha Mifumo ya Gridi-Eastern Africa Power Pool (EAPP).
Sambamba na hilo, makatibu wakuu hao walisisitiza umuhimu wa kuongeza wigo wa njia za usafirishaji umeme zitakazounganisha nchi hizo mbili kupitia maeneo ya Namanga, Lungalunga, Loitoktok na Isibania/Sirari.
Aidha, kikao hicho kilijadili pendekezo la kuanzishwa kwa mfumo wa ‘Ring Circuit’ utakaojumuisha njia za Ibadakuli-Masaka, Ibadakuli-Kilgoris na Kilgoris-Masaka kwa lengo la kuongeza uthabiti wa gridi za umeme na kuimarisha biashara ya umeme kati ya Tanzania na Kenya.
Katika hatua nyingine, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Mafuta wa Kenya, Alex Wachira alieleza kuwa nchi hiyo imejipanga pia katika uwekezaji wa miundombinu ya gesi asilia kwa lengo la kuimarisha upatikanaji wa nishati hiyo nchini humo na kuongeza ushirikiano wa kikanda katika sekta ya nishati.
Aidha, Kenya ilieleza uzoefu wake katika biashara ya umeme wa kikanda, ikibainisha kuwa inaendelea kupokea umeme kutoka Ethiopia kupitia mikataba ya biashara ya umeme ya kikanda, ambapo kiwango cha umeme hupungua na kuongezeka kulingana na mahitaji, huku kikifikia takriban megawati 100 katika vipindi vya kawaida.
Hatua hiyo imeelezwa kusaidia kuimarisha uthabiti wa mfumo wa umeme Kenya.
Kikao hicho kilihudhuriwa na viongozi na wataalamu mbalimbali kutoka wizara za nishati za Tanzania na Kenya pamoja na taasisi za sekta ya umeme ikiwemo TANESCO, KETRACO na KPLC.



