Na MWANDISHI WETU
TIMU ya Simba, imekaa kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara, baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 mbele ya Coastal Union, katika mchezo uliofanyika Uwanja Mkwakwani, jijini Tanga.
Simba imekaa kileleni mwa msimamo wa michuano hiyo kufuatia kufikisha pointi 55, nyuma ya Yanga yenye pointi 54 nafasi ya pili huku Azam ikishikilia nafasi ya tatu kwa pointi zake 46.
Baada ya ushindi wa jana, Wekundu wa Msimbazi, wameishusha Yanga kileleni huku wana Jangwani hao wakiwa na mchezo mmoja mkononi.
Mchezo huo, ulianza kwa kasi, timu zote zikishambuliana kwa zamu kila mmoja ikitaka bao la mapema ili kujiweka katika mazingira mazuri.
Katika dakika ya nane, Coastal Union ilifanya shambulizi la kushtukiza ambapo Maabad Maulid alifunga bao la kuongoza baada ya kufumua shuti kali lililojaa wavuni kufuatia mabeki wa Simba kujichanganya.
Simba walijibu shambulizi, dakika ya 25 Elie Mpanzu alipata nafasi lakini shuti lake lilitoka sentimeta chache nje ya lango kabla ya Anicet Oura kurudia kosa kama hilo dakika ya 29.
Katika dakika ya 36, Libasse Gueye aliwainua katika viti mashabiki wa Simba baada ya kusawazisha bao la kwanza kwa shuti kali la mguu wa kustoto kufuatia kazi nzuri iliyofanywa na Clatous Chama.
Simba ilipata bao la pili dakika ya 44 likiwekwa kimiani na Libasse baada ya kuunganisha kwa kichwa kona iliyochongwa na Chama, hadi mapumziko ya kipindi cha kwanza, Simba ilikuwa mbele kwa mabao 2-1.
Kipindi cha kilianza kwa kasi, timu zote zikifanya mashambulizi ya hapa na pale, dakika ya 62, Meshack Mwamita aifungie bao Coastal Union ambapo aligonga kichwa mpira ukatoka nje.
Dakika ya 70, kipa wa Coastal Union, Chuma Ramadhani alifanya kazi ya ziada kuokoa shuti la Seleman Mwalimu akiwa ndani ya eneo la hatari na baadaye kugonga kichwa mpira ukapaa juu ya lango, krosi ilitoka kwa Mpanzu.
Mpira uliendelea kwa kasi huku mashambulizi yalifanyika kwa kupokezana, hadi mchezo unamalizika, Simba iliibuka kidedea kwa ushindi wa mabao 2-1.
Hata hivyo, Chama ameendelea kung’ara baada ya kubeba tuzo ya mchezaji bora wa mechi kwa mara ya tano mfululizo kufuatia kuhusika moja kwa moja katika mabao ya Simba katika mchezo huo.
Katika hatua nyingine, JKT Tanzania jana ililazimishwa sare ya mabao 2-2 dhidi ya Fountain Gate, katika mchezo uliofanyika Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Mbweni, Dar es Salaam.
Coastal Union:Chuma Ramadhani, Jofrey Manyac, Ally Msangi, Andrew William, Aidan Alexander, Bakari Selemani, Saad Mwanza, Christopher Oruchum, Shiza Kichuya, Gradi Kiala na Maabad Maulid.
Simba: Mahamadou Kassali, David Kameta, Libasse Gueye, Yusuph Kagoma, Rushine De Reuck, Kante Alasane, Nickson Kibabage, Anicet Oura/ Seleman Mwalimu, Ismael Toure, Elie Mpanzu na Clatous Chama/ Inno Loemba.




