Na AMINA KASHEBA
PAMOJA na Tanzania kufuzu nusu fainali katika michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika , Kocha wa timu ya taifa kwa wachezaji wenye umri chini ya miaka 17 ‘Serengeti Boys’, Elieneza Nsanganzelu, amedai kuwa mchezo dhidi ya Algeria ulikuwa na upinzani mkubwa.
Serengeti Boys ilishinda kwa mikwaju ya penati 4-3 dhidi ya Algeria, baada ya timu hizo kutoka sare 3-3 ndani ya dakika 90, katika mtanange uliopigwa Uwanja wa Mohammed XVI, Rabat nchini Morocco.
Kutokana na matokeo hayo, Serengeti Boys itaumana na Misri katika mechi ya nusu fainali kutafuta nafasi ya kucheza fainali.
Nsanganzelu alisema katika mchezo huo, kikosi chake kilikabiliwa na upinzani mkali uliotokana na kiu ya kuitoa Tanzania ambayo ni timu tishio katika mashindano.
“Ilikuwa mechi ambayo wapinzani nao walitaka ushindi, pamoja na Algeria kuwa na vijana wengi wanaocheza soka barani Ulaya, wachezaji wangu walijipanga kuwaonyesha kuwa ni bora zaidi yao,” alisema.
Kocha huyo alisema baada ya kusonga mbele, anajua kuwa mchezo wa nusu fainali utakuwa mgumu zaidi lakini anaiandaa timu kupata matokeo mazuri zaidi na kucheza fainali.
“Tunaenda kufanyia kazi kasoro zote zilizojitokeza katika mechi za makundi na robo fainali, sasa mguvu zote tumeelekeza katika mchezo wa nusu fainali,” alisisitiza.
Nahodha wa Serengeti Boys, Kassim Juma, alisema mechi ilikuwa ngumu kwani Algeria ilitoa upinzani mkali.
Mchezaji huyo aliwaomba Watanzania kuendelea kuwasapoti kwani hatua ya nusu fainali waliyofikia ni kubwa tofauti na walipotoka, wanahitaji maombi kwa ajili ya kufika fainali.
“Haikuwa kazi nyepesi ni kitu cha kujitolea kwa sababu wapinzani walijipanga kuhakikisha wanashinda, lakini sisi tulisikiliza maelekezo ya walimu wetu,” alisema.
Serengeti Boys tayari imeshafuzu kucheza michuano ya fainali za Kombe la Dunia itakayofanyika nchini Qatar kuanzia Novemba 19 hadi Desemba 13, mwaka huu baada ya kutinga robo fainali ya michuano hiyo.




