Na MWANDISHI WETU
RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, amewataka Majaji wa Mahakama ya Rufani aliyowateua, kufanya kazi kwa uadilifu, weledi, busara na hofu ya Mungu kama viapo vyao vinavyowataka.
Rais Samia, alitoa maagizo hayo alipowaapisha Majaji wateule wa Mahakama ya Rufani aliowateua hivi karibuni, katika hafla iliyofanyika Ikulu jijini Dar es Saalam.
Pia, Rais Samia, aliwataka Majaji hao kuimarisha uwajibikaji, nidhamu na maadili ndani ya mhimili huo muhimu.
“Mahakama ya Rufani ndiyo ngazi ya juu kabisa kwa utoaji wa haki katika nchi yetu, kwa hiyo, kila uamuzi mnaotoa una uzito mkubwa si kwa wahusika na washauri pekee, bali kwa taasisi zetu na tafsiri pana ya sheria ya nchi yote inawaangalia ninyi kama wasimamizi wa haki kwenye taifa letu,” alisema Rais Samia.
Aliwasisitiza Majaji hao kulinda heshima na uhuru wa Mahakama, waendelee kuimarisha uwajibikaji na nidhamu.
“Uhuru huu unakwenda sambamba na uadilifu, ufanisi na utendaji wenu unaoangalia pia uzalendo kwa nchi yenu na kutoa maamuzi ya taifa kwanza, nchi kwanza halafu mtakwenda kwenye mambo mengine,” alisema.
Alisema uteuzi wa Majaji hao ni ishara kwamba, wamefanya kazi nzuri na Tume ya Utumishi wa Mahakama, imetambua kazi zao na imewapendekeza kupandishwa katika ngazi hiyo.
“Ni imani yangu kwa heshima hiyo mliopewa, mtafanya kazi kwa bidii zaidi, nendeni mkaongeze nguvu katika Mahakama ya Rufani kwa kutambua umuhimu wa haki kama msingi wa amani, utulivu lakini maendeleo ya taifa letu na ustawi wa wananchi wetu kwa ujumla.
“Mmeapa mtafanya kazi bila upendeleo, huba, chuki hasa bila upendeleo kwa sababu kazi zenu zina sheria zake, kuna haka kahuba na kachuki, sijui ndicho ninachotaka mkajitazame vizuri ndani yenu katika kutoa maamuzi ya hukumu zenu,”alisema.
Alisema dhamana hiyo si ya cheo tu, ni wajibu wa kulinda haki za Watanzania, hivyo katika uamuzi wote wanaofanya, wanapaswa kukumbuka kauli ya kuwatumikia wananchi, sawa na kumtumikia Mungu.
“Mnafanya kazi kubwa ya nchi, mna dhima kubwa ya kutenda haki kuhakikisha haki za wananchi zinapatikana, lakini hata haki ya kusimamia taifa lenu, iko mikononi mwenu.
“Kwa muktadha huo, uteuzi wenu wa kuwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, ni sehemu ya jitihada hizo za kuongeza ufanisi katika mhimili huu muhimu.
“Tumefanya mengine mengi na ninyi mashahidi kwamba, mahakama zimebadilika kwa kiasi kikubwa na zimeendelea kwa kiasi kikubwa katika miaka ya hivi karibuni,”alisema.
Mei 20 mwaka huu, Rais Dk. Samia, alifanya uteuzi wa Majaji tisa wa Mahakama Kuu kuwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, wakiwemo Majaji saba kutoka Mahakama Kuu ya Tanzania na wengine wawili wa Mahakama Kuu ya Zanzibar.
Walioteuliwa ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Dodoma, Abdi Shaaban Kagomba na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Arusha, Yohane Bokobora Masara.
Mbali na hao, wengine ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Bukoba, Immaculata Kajetan Banzi na Jaji wa Mahakama Kuu ya Zanzibar, Rabia Hussein Mohamed.
Wengine ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara, Dar es Salaam, Cyprian Phocas na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Dar es Salaam, Dk. Yose Joseph Mlyambina.
Wengine ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Kuu Dodoma, Iman, Daud Aboud, Jaji wa Mahakama Kuu ya Zanzibar, Mzee Ibrahim Ibrahim na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Dodoma, Dk. Juliana Laurent Masabo.




