IRENE MWANSOMOLA Na EMMANUEL MOHAMED
RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, amezialika taasisi za fedha na wawekezaji kuangalia fursa zilizopo nchini, katika sekta za usafirishaji, nishati, usafirishaji wa bidhaa, uzalishaji viwandani, miundombinu ya kidijitali na maendeleo ya viwanda.
Kauli hiyo aliitoa, wakati akifungua Mkutano wa Wanahisa wa Africa50 na Jukwaa la Miundombinu, uliofanyika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Saalam.
Rais Samia, alisema Tanzania siyo eneo la kuzalisha malighafi tena, bali ni eneo la uwekezaji kwa ajili ya uongezaji thamani, ubunifu na uzalishaji wa viwandani.
“Kwa upande wetu sisi Tanzania, mabadiliko ya miundombinu yetu yanaongozwa na Dira ya Maendeleo ya Tanzania 2050 kwa kipindi cha miaka 25 ijayo, ambayo utekelezaji wake ulianza Julai, mwaka huu.
“Dira hiyo, inaainisha azma yetu ya kujenga uchumi wa ushindani wa viwanda unaojumuisha makundi yote ya jamii, unaoendeshwa na ubunifu, rasilimali watu, maendeleo endelevu na miundombinu ya kisasa,” alisema.
Rais Samia, alisema Tanzania inatambua mabadiliko hayo hayawezi kufikiwa na serikali pekee kuelekea Dira 2050, hivyo imeweka sekta binafsi kuwa kiini cha ukuaji wa uchumi. Sekta binafsi imepewa asilimia 70 kutekeleza Dira hiyo.
“Jukumu letu kama serikali ni kuweka mazingira ya uwekezaji yenye kutabirika, kutekeleza miundombinu ya kimkakati ya umma na kujenga ushirikiano utakaofungua fursa kwa mitaji ya sekta binafsi, ubunifu na ujasiriamali.
“Katika miaka iliyopita, Tanzania imeendesha miradi mikubwa ya maendeleo ya miundombinu ambayo ni miongoni mwa juhudi kubwa zaidi katika historia ya nchi yetu,”alisema.
Rais Samia, alisema Tanzania imepanua na kufanyia uboreshaji Bandari ya Dar es Salaam, hatua iliyoongeza ufanisi na kuimarisha nafasi yake kama kitovu cha biashara na usafirishaji wa bidhaa katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.
“Pia, tunaendeleza ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) ili kuboresha muunganiko wa usafirishaji, kupunguza gharama za usafiri na kurahisisha biashara na nchi jirani.
“Lakini, tunawekeza katika barabara za kimkakati, mtandao wa barabara, madaraja, korido za usafirishaji wa bidhaa na viwanja vya ndege vya kisasa, tukiwa na lengo la kuimarisha miundombinu ya kimataifa na kikanda,”alisema.
Katika maelezo yake, Rais Dk. Samia, alisema uwekezaji huo, umeanza kuleta matokeo kwa kupunguza gharama za usafirishaji.
“Uwekezaji huu, unaendelea kuimarisha nafasi ya Tanzania kama lango muhimu la nchi zisizo na bandari, zikiwemo Burundi, Rwanda, Uganda, Zambia, Malawi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), kwa kuzipatia fursa ya kufikia masoko ya kikanda na kimataifa kwa ufanisi.
Alisema kupitia uwekezaji endelevu katika miundombinu, Tanzania inaendelea kuimarisha nafasi ya kuunganisha masoko, kurahisisha biashara na kusaidia ushirikiano wa kikanda.
“Kama mwanachama hai wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), Tanzania ina nafasi ya kipekee ya kuwa daraja linalounganisha jumuiya hizi mbili muhimu za kikanda.
“Tumejizatiti kutumia nafasi hii kuimarisha biashara ya kuvuka mipaka, kuendeleza minyororo ya thamani ya kikanda na kukuza uwekezaji unaoleta ustawi wa pamoja,”alisema.
Rais Samia, alisema serikali inaendelea kuimarisha miundombinu ya kidijitali kupitia Mkongo wa Taifa wa mawasiliano kwa lengo la kuleta mageuzi nchini.
Alizitaka sekta binafsi kushirikiana na serikali kutekeleza miradi kwa kuwa, bado Afrika ina changamoto ya rasilimali fedha.
WAZIRI WA FEDHA
Naye Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar, alisema Jukwaa la Africa50, litachochea mabadiliko katika utekelezaji wa miradi.
Balozi Omar alisema Rais Samia, amefanikisha Tanzania kuwa na ubia na nchi mbalimbali katika sekta tofauti.
WAZIRI NDEJEMBI
Waziri wa Nishati, Deogratius Ndejembi, alisema matumzi ya nishati safi nchini, yameongezeka kutoka asilimia sita mwaka 2021 hadi asilimia 20 mwaka huu.
Ndejembi, alisema mafanikio hayo, yametokana na jitihada za Rais Samia, aliitaka Afrika kushirikiana kutengeneza miundombinu inayotoa fursa za kufanikisha matumizi ya nishati safi.
MKURUGENZI AFRICA50
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Africa50, Alain Ebobiss, alimpongeza Rais Samia kufanikisha Tanzania kuingia katika Africa50.
Mkurugenzi huyo, alisema Tanzania kupitia jukwaa hilo, Afrika itajielekeza kutekeleza miradi na kukuza viwanda.
Ebobiss, alisema upatikanaji nishati unahitajika katika utekelezaji wa miradi, ambapo Afrika inatarajia kuzindua Jukwaa la Uwekezaji wa Gesi.
Aidha, Mkurugenzi huyo alisema watatumia Jukwaa la Africa50 kushirikiana katika utekelezaji wa miradi, kwa sababu miundombinu ya Afrika ni fursa kubwa ya uwekezaji.
Alisema Africa50 ilianzishwa kuwa na miradi ya kibenki, lakini hivi sasa maono hayo yamejenga taasisi zilizoleta mabadiliko ya kiuchumi.
Alisema tangu kuanza Africa50, jukwaa hilo limesaidia uwekezaji wa thamani ya zaidi ya Dola za Marekani bilioni tisa.
RAIS BENKI YA AfDB
Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Dk. Sidi Ould Tah, alisema benki hiyo itashirikiana vyema na Africa50 kuwezesha upatikanaji wa fedha.
Pia, alisema Tanzania imekuwa mbia mkubwa katika sekta ya miundombinu barani Afrika na alimpongeza Rais Samia kufanikisha Tanzania kuingia Jukwaa la Afrika50.
MAKAMU WA RAIS KENYA
Makamu wa Rais wa Kenya, Kithure Kindiki, alitoa rai kwa nchi za Afrika kushirikisha sekta binafsi kufanikisha ujenzi wa miundombinu.
Kindiki alidokeza Afrika inahitaji kutumia ubunifu katika kugharimia miradi na kutumia rasilimali za ndani ya nchi na kikanda.
Aliongeza kuwa, Afrika inahitaji kujipanga katika sekta ya nishati, akitoa mfano bomba la mafuta linalotoka Msumbiji ni vyema kufika na Kenya.
Kindiki, alisema nishati ni muhimu katika mendeleo ya viwanda na inahitajika kwa bei nafuu kwalengo la kuwafikia wananchi wengi.
Alisema miundombinu ya kutosha inahitajika kwa ajili ya kusambaza nishati hiyo iwafikie watu nyumbani na kuendesha viwanda.
Alieleza kuwa, bara la Afrika lina hifadhi kubwa ya gesi katika nchi mbalimbali zikiwemo Senegal, Nigeria na Tanzania.
Kindiki alisema Afrika lazima ijenge uthubutu na kuamini uwezo wake katika kufanya mambo ambayo nchi zingine zimefanya.
Alisema wakati nchi za Afrika zinaendelea kujijenga kidemokrasia ni lazimamafanikio yaende pamoja na mabadiliko hayo.
Aidha, Kindiki alitoa rai kwa nchi za Afrika kuwa na siasa zinazojenga nchi kwa maendeleo.
TANZANIA YATIA SAINI MIKATABA
Katika hatua nyingine, Tanzania imetia saini mikataba mitatu ya makubaliano (MoU) na Afrika 50 katika sekta ya afya upande wa usafishaji wa figo, usambazaji wa nishati ya umeme na gesi asilia.
Mikataba hiyo, ilisaniwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dk. Grace Maghembe, Kaimu Mkurugenzi Mkuu Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Timothy Mgaya, Waziri wa Nishati, Deogratius Ndejembi, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Maendeleo Petroli Tanzania (TPDC), Mussa Muhammed Makame.




