Na MWANDISHI WETU
WAKATI Ligi Kuu Tanzania Bara ikizidi kupamba moto, timu ya JKT Tanzania ndiyo kinara wa kupachika mabao hadi sasa msimu huu.
JKT Tanzania ambayo ndiyo kinara wa ligi hiyo, imepachika mabao 10 katika mechi nane ilizocheza hadi sasa msimu huu.
Katika ligi hiyo, JKT Tanzania imevuna pointi 13 huku ikiruhusu mabao manane katika nyavu zake.
Kikosi hicho kinafuatiwa na Yanga iliyofunga mabao tisa katika mechi nne, ikiruhusu bao moja na kushika nafasi ya tatu katika msimamo baada ya kuvuna pointi 10.
Simba iliyopo katika nafasi ya tano katika msimamo wa ligi baada ya kuvuna pointi tisa katika mechi tatu, imefunga mabao manane na kuruhusu moja.
Timu hizo zinafuatiwa na Mbeya City iliyopachika mabao saba, Namungo iliyofunga mabao sita, Mashujaa iliyofunga mabao matano, Pamba Jiji iliyopachika mabao matano, Coastal Union iliyofunga mabao matano na Dodoma Jiji iliyopachika mabao matano.




