Na MWANDISHI WETU
SIKU chache baada ya Bunge la Umoja wa Ulaya (EU) kuazimia kuzuia kwa muda kutia saini mikataba ya fedha za ubia kwa mwaka 2025, Serikali imeweka bayana kuwa, uamuzi huo, hautakuwa na athari kubwa kwa bajeti kuu ya serikali.
Serikali imesema sehemu kubwa ya fedha hizo ni za Programu ya Ushirikano na EU kwa mwaka 2025, siyo kwa ajili ya Bajeti ya Serikali Kuu (Budget Support) na kwamba, hazitarajiwi kuingizwa katika Mfuko Mkuu wa Serikali.
Imewataka wananchi kutotishwa na taarifa za upotoshaji, zinazotolewa na vyanzo mbalimbali, ikiwemo mitandao ya kijamii.
Ufafanuzi huo, ulitolewa kupitia taarifa ya serikali kwa vyombo vya habari, iliyotolewa na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.
“Suala lingine linalopotoshwa ni kuhusu ukubwa wa madhara ya uamuzi huu, hususani kwenye Bajeti ya Serikali.
“Usahihi ni kwamba, kiasi cha Euro Milioni 156 kwenye Programu ya Ushirikano na EU kwa mwaka 2025, siyo kwa ajili ya Bajeti ya Serikali Kuu (Budget Support), wala hazitarajiwi kuingizwa kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali.
“Fedha hizo zinaenda wapi? Kwa ujumla, fedha hizo zimepangwa katika miradi mitatu mikuu; Mradi wa Together4Value. Mradi huo wenye jumla ya Euro milioni 129, unalenga kuimarisha minyororo ya thamani katika sekta za madini na kilimo.
“Kati ya fedha hizi, ni Euro milioni 13 pekee ndizo ambazo zinakwenda moja kwa moja kwenye taasisi za Serikali (Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji), sawa na asilimia 16 ya mradi wote.
“Sehemu kubwa ya fedha, takribani Euro milioni 116 zitasimamiwa kupitia utaratibu wa ‘indirect management’ kupitia mashirika ya nchi wanachama wa EU, taasisi za ndani na kimataifa na kampuni za ushauri,” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kuwa, eneo lingine ni Mradi wa Uchumi wa Kidijitali Tanzania na Uunganishaji (Tanzania Digital Economy and Connectivity Initiative (TANTECH), wenye thamani ya Euro milioni 20, ulibuniwa kuchochea maendeleo ya uchumi wa kidijitali na ubunifu.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, kati ya fedha hizo, Euro milioni 1.5 ambazo ni sawa na asilimia 7.5 ya bajeti yote ndizo zimepangwa kwenda moja kwa moja serikalini kupitia Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari.
Fedha zilizobaki takribani Euro milioni 18, zitaelekezwa kupitia mfumo wa ‘indirect management’ katika taasisi za nchi wanachama wa EU, NGO na sekta binafsi.
Aidha, Mfuko wa Ushirikiano (Cooperation Facility), ulitengewa Euro milioni saba, unaolenga kuimarisha uratibu wa ushirikiano kati ya Tanzania na EU.
Katika mradi huo, Euro milioni 2.5 sawa na asilimia 35, ndizo zimepangwa kwenda serikalini kupitia Wizara ya Fedha na Tume ya Mipango.
“Kiasi kilichobaki takribani Euro milioni 4.5, kimepangwa kutekelezwa kupitia wataalamu elekezi na taasisi za ndani za kimataifa katika mfumo wa ‘indirect management’.
“Kwa mnyumbuliko huu, kati ya Euro milioni 156 za AAP 2025, ni Euro milioni 17 tu (sawa na asilimia 10.9), ndizo ambazo zinakwenda moja kwa moja kwenye miradi inayotekelezwa na taasisi za serikali.
“Zaidi ya Euro milioni 138.6 (asilimia 89.1), zimepangwa kutekelezwa kupitia mfumo wa ‘indirect management’ unaohusisha mashirika ya sekta binafsi kwa kushirikiana na mashirika ya EU, mashirika ya kimataifa, NGO, kampuni za ushauri za kimataifa,” ilifafanua taarifa hiyo.
Ilisema ni sehemu ndogo ya fedha hizo itakayoelekezwa katika miradi ya baadhi ya taasisi za serikali, huku sehemu kubwa ikitarajiwa kuekelezwa kwa wadau mbalimbali nje ya serikali, hususan sekta binafsi ya Tanzania kwa ushirikiano na baadhi ya sekta binafsi ya Ulaya, mashirika ya kimataifa, asasi za kiraia na taasisi za ndani na kimataifa za ushauri wa kitaalamu (consultancies).
“Kwa hiyo, hatua yoyote ya kuchelewesha kusaini fedha hizi, haiathiri serikali pekee,” ilieleza.
Hata hivyo, ilisema kwa kuzingatia manufaa tarajiwa katika programu hiyo kati ya wadau wa ndani na nje, serikali pamoja na EU, zitaendeleza majadiliano kwa haraka kuwezesha utiaji saini programu hizo kufanyika mapema kadri inavyowezekana kuepuka athari zinazoweza kujitokeza kwa wadau mbalimbali.
ilisema ni vizuri ikaeleweka kwamba, masuala ya kimahusiano kati ya Tanzania na EU, yanasimamiwa na Kamisheni ya Umoja wa Ulaya, siyo Bunge.
Hivyo, lolote linaloazimiwa na Bunge la Ulaya, linapaswa kufanyiwa uamuzi mwingine na kamisheni hiyo ili kama kuna jambo la kufikishwa kwa serikali kufanya majadiliano, yanapaswa kufikishwa na kamisheni hiyo kwa kuwa, ndicho chombo rasmi kinachosimamia mahusiano ya kidiplomasia baina ya Tanzania na EU.
“Hivyo, Watanzania wapuuze taarifa potofu zinazojaribu kuchukua vipengele vya maazimio ya Bunge la EU kama masharti yanayoelekezwa kwetu na kwamba, lazima tuyatekeleze mara moja.
“Hakuna kitu kama hicho. Ni lazima jambo lolote lipate mwafaka kwenye majadiliano.




