Arusha
NA LILIAN JOEL
RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika mkutano wa Umoja wa Mabunge Duniani (IPU) unaotarajiwa kufanyika mwakani jijini Arusha ambao utahudhuriwa na wageni zaidi ya 1500 kutoka mataifa mbalimbali.
Hayo yalibainishwa jijini hapa, baada ya ujumbe wa IPU ukiongozwa na Balozi Ande Filip ulipokutana na Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Amos Makalla, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya mkutano huo.
Balozi Ande alisema mkutano huo utahudhuriwa maspika, wabunge na viongozi zaidi ya 1500 kutoka mataifa mbalimbali duniani ambapo Rais Dk. Samia anatarajiwa kuwa mgeni rasmi.
“Kulingana na ratiba, washiriki tutakuwa hapa kwa zaidi ya siku sita ambapo baada ya kumalizika kwa mkutano, watapata fursa kutembelea maeneo ya kihistoria na vivutio vya utalii vilivyopo Mkoa wa Arusha,” alieleza.
Awali, akiukaribisha ujumbe huo, Makalla alisema Tanzania itakuwa mwenyeji wa mkutano huo kwa sababu ya ushiriki na historia yake katika Bunge la IPU.
“Sisi tumewahakikishia tupo tayari kuwa wenyeji wa mkutano huo, tupo tayari kuwapa ushirikiano kufanikisha mkutano huo mkubwa wa kihistoria.
“Tanzania ni Mwenyeji kwa sababu ya ushiriki wake wa historia katika IPU. Kikubwa zaidi ni namna wao wanavyoiona Tanzania, sisi tumewahakikishia tupo tayari kuwapa ushirikiano kufanikisha mkutano huo mkubwa,” alieleza.
Alisisitiza: “Hii ni fursa kwetu kwa Tanzania kuendelea kuaminika kimataifa. Niwaombe wananchi kujiandaa kutumia fursa za ujio wa mkutano huo kiuchumi.”




