Na ABDUL DUNIA
PAMOJA na kupata ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Mbeya City, Kaimu Kocha Mkuu wa Simba, Selemani Matola, amesema bado ana kazi kubwa ya kufanya kuhakikisha washambuliaji wake wanatumia vyema nafasi zinazotengenezwa.
Simba ilipata ushindi huo katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara uliopigwa Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Dar es Salaam.
Katika mtanange huo ambao Mbeya City ilimaliza pungufu kwa straika wake Vitalis Mayanga kuonyeshwa kadi nyekundu dakika ya 28, Simba ilikosa nafasi nyingi za wazi.
Kuhusu ukosaji wa nafasi za wazi, Matola alikiri huku akisema kwamba, ana kazi kubwa ya kufanya kwa nyota wake kuhakikisha wanakuwa makini katika eneo la mwisho.
“Ninafikiri ni tatizo letu kubwa kutumia nafasi, tuna kazi kubwa sana ya kubadilisha nafasi kuwa magoli,” alisema.
Hata hivyo, Matola aliipongeza timu yake kwa ushindi huo huku akisema ni jambo zuri kwenda kuchuana na Azam FC kesho wakiwa wametoka kupata ushindi.
“Ni kitu kizuri, imetupa nguvu kubwa kuelekea katika dabi ya Mzizima, haitakuwa mechi rahisi lakini ni jambo zuri kupata ushindi tukielekea katika dabi,” alisema.
Simba itachuana na Azam FC kesho katika Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.
Katika michuano hiyo, Simba ipo nafasi ya tano kwa alama 12 katika mechi nne, ikifunga mabao 11 na kuruhusu moja huku Azam FC ikiwa nafasi ya 12 kwa alama sita katika mechi nne, ikifunga mabao manne na kuruhusu mawili.




