Na NASRA KITANA
BODI ya Wakurugenzi wa klabu ya Simba, imekaa kikao kizito kufanya mchujo wa maombi ya makocha zaidi ya 100 wanaotaka nafasi hiyo.
Simba inasaka kocha mpya baada ya kumtema Dimitar Pantev aliyetambulishwa kama meneja akiitumikia kwa siku 61 baada ya kuwa na mwenendo mbaya ndani ya kikosi chao.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi, Meneja wa Habari na Mawasiliano Simba, Ahmed Ally alisema kuwa mchakato wa kusaka kocha mpya unaendelea na hivi sasa viongozi wanachakata maombi yaliyotumwa.
“Kuna maombi mengi ya makocha kutoka nchi mbalimbali wakitaka kuifundishia Simba, lakini viongozi watahakikisha wanachagua kocha mwenye CV nzuri kuweza kuifundishia Simba.
“Hadi sasa tumepokea maombi zaidi ya 100 hivyo kazi kubwa inaendelea ya kuchakata maombi hayo, tupate kocha bora mwenye viwango vya kimataifa,” alisema.
Ahmed aliongeza kuwa kwa kipindi hiki, wanahitaji kocha bora na imara ambaye ataisaidia timu yao kuweza kufikia malengo waliojiwekea katika Ligi Kuu Tanzania Bara na michuano ya Ligi ya Mabingwa Barani Afrika.
Alifafanua kuwa hali hiyo, inatokana na timu yao kuwa na ngumu kwa kipindi hiki hivyo mashabiki na wapenzi wa timu yao wanatakiwa kutulia wakati timu inatafuta suluhisho litalokuwa bora.
Hata hivyo, taarifa za ndani zinaeleza kuwa Simba imeanza mazungumzo na makocha Antonio Casano Cantos kutoka Hispania akiwa na sifa za kufundisha soka nchi za Angola na Morocco.
Pia, kupitia timu za Petro Atletico na Moghreb Atletico Tetouan na Steve Barker wa Stellenbosch ya Afrika Kusini.
Lakini Meneja wa Habari na Mawasiliano Simba, Ahmed Ally alishindwa kueleza kwa undani juu ya kuwepo habari hizo.
Wakati huo huo, dirisha dogo la usajili linatarajiwa kufunguliwa Januari Mosi, mwakani na Simba imepanga kusikilizia mapendekezo ya kocha mpya au Seleman Matola kama atapenya kisha kujiweka tayari kwa mechi nne za Ligi ya Mabingwa Afrika hatua ya makundi ikiwemo michezo miwili ua nje na ndani dhidi ya Esperance ya Tunisia.
Simba ipo Kundi D, mbali na Esperance pia zipo Stade Malien ya Mali na Petro Atletico ya Angola ikisaka nafasi ya kucheza robo fainali kwa mara ya saba tangu 2018-2019.




