Na NASRA KITANA
WACHEZAJI wa timu ya Taifa ‘Taifa Stars’, Idd Seleman ‘Nado’ na Hussein Masalanga wamesema wapo tayari kupambana kuhakikisha Tanzania inafanya vizuri katika fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2025).
Wakizungumza kwa nyakati tofauti, wachezaji wa timu hiyo, walisema wapo tayari kwa ajili ya vita ya kusaka taji hilo na kuwapa furaha Watanzania.
Idd Selemani ‘Nado’, alisema kuwa kwanza ni furaha kwake kushiriki AFCON kwa mara ya kwanza na atahakikisha anapambana ili kufunga mabao katika mashindano hayo.
Alifafanua kuwa kila mchezaji ana shauku kubwa ya kuipambania timu yao na jinsi wanavyoendelea kupata mafunzo kutoka kwa Kocha Miguel Gamondi.
“Kwanza niseme, kambi yetu ni nzuri na mwalimu amekuwa akitupa mbinu tofauti tofauti kuhakikisha tunashinda katika kila mchezo, kwa upande wangu kitu kinachotakiwa ni kuifungia timu yangu mabao, naamini hii itakua nafasi nzuri ya kuonesha kipaji changu,” alisema Nado.
Mchezaji huyo alisema kuwa timu yao inaendelea kufanya mazoezi kwa bidii, wachezaji wote wako katika ari kubwa ya kushindana na kuipatia heshima Tanzania.
Kipa wa timu hiyo, Hussein Masalanga alisema wachezaji wote wanafanya mazoezi kwa bidii, kujiandaa ipasavyo na mashindano hayo yatakayofanyika nchini Morocco.
Masagala alisema kwa upande wa makipa wanaendelea kujipanga ili kuwa bora na kutoruhusu mabao katika mashindano hayo.
“Mashindano haya ni makubwa kwa Afrika, hivyo sisi wachezaji hatutakubali kuwa wanyonge, tunaendelea kufanya maandalizi ya kutosha ili tuwe katika kiwango bora na kutimiza malengo tuliyojiwekea,” alisema Masagala.
Hii ni mara ya nne, Stars kufuzu fainali za AFCON ikishiriki mara ya kwanza mwaka 1980 nchini Nigeria, mwaka 2019 michuano iliyofanyika nchini Misri na mwaka 2023 ilichezwa nchini Ivory Coast.




