NA MWANDISHI WETU
MKURUGENZI mteule wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF), Fortunatus Magambo, ameahidi kuendeleza mafanikio yote yaliyoanzishwa na mtangulizi wake kwa maslahi mapana ya Taifa, wanachama na wananchi kwa ujumla.
Magambo ameyasema hayo Desemba 16, 2025, wakati wa hafla ya kukabidhiwa ofisi rasmi na aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa PSSSF, Dk. Rhimo Nyansaho, ambaye kwa sasa ni Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa.
Akizungumza katika hafla hiyo, Magambo amemshukuru Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, kwa kumuamini na kumteua kuiongoza PSSSF na kuwapongeza watangulizi wake kwa kazi kubwa waliyoifanya katika kuimarisha Mfuko huo.
“Kwa kushirikiana na wenzangu, nitahakikisha tunaendeleza kazi nzuri zilizofanyika, kwa lengo la kuhakikisha wanachama wetu, hususan wastaafu, wanapata huduma sahihi na kwa wakati,” amesema Magambo.
Kwa upande wake, aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa PSSSF, Dk. Nyansaho, aliwataka watumishi wa Mfuko huo kuendelea kutendeana mema, akisema hatua hiyo itaongeza morali ya kazi na kuchangia utoaji wa huduma bora kwa wanachama.
Dk. Nyansaho pia aliishauri menejimenti ya PSSSF kuwekeza katika miradi yenye tija kwa Mfuko na Taifa kwa ujumla, hususan miradi inayozalisha ajira kwa vijana na kutoa soko kwa bidhaa zinazozalishwa na Watanzania.
Aidha, ameitaka menejimenti kuhakikisha watumishi wanaendelea kufanya kazi katika mazingira salama na yenye furaha, akiwashukuru kwa ushirikiano waliompatia kipindi chote cha uongozi wake.
Dk. Nyansaho ameteuliwa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kuwa Mbunge na baadaye kuteuliwa kuwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa.




