NA MWANDISHI WETU
KATIKA siku za hivi karibuni, kumebainika kuwepo kwa utendaji usioridhisha katika Hospitali ya Temeke, ikiwemo kuzimwa kwa mashine ya X-Ray pamoja na vitendo vya rushwa vinavyodaiwa kufanywa bila uoga.
Ufuatiliaji wa siri uliofanywa na Waziri wa Afya, Mohamed Mchengerwa, umebaini kuwa baadhi ya walinzi na watoa huduma wanahusika na vitendo hivyo, sambamba na kutoa kauli zisizo za staha kwa wagonjwa.
Imeelezwa kuwa baadhi ya watumishi hao wamekuwa wakiwafokea na kuwadharau wagonjwa, hali inayokiuka maadili ya kazi na misingi ya utoaji wa huduma za afya.
Kufuatia hali hiyo, Waziri Mchengerwa amemuelekeza Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dkt. Seif Shekalaghe, kufanya uchunguzi wa kina katika hospitali hiyo ili kubaini chanzo cha changamoto hizo na kuwachukulia hatua za kisheria na kinidhamu watakaobainika kuhusika, kwa mujibu wa sheria na kanuni za utumishi wa umma.
Aidha, Waziri Mchengerwa ametoa wito kwa watumishi wote wa sekta ya afya nchini kubadilika na kuzingatia maadili ya kazi, akisisitiza kuwa Serikali haitasita kuchukua hatua kali dhidi ya watumishi wazembe, wala rushwa au wanaokiuka misingi ya maadili ya utumishi.




