Na NASRA KITANA
SIKU moja baada ya Paul Makonda kuteuliwa kuwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, wadau wa michezo nchini wamemtumia salamu na kusisitiza kufurahishwa na uteuzi wake.
Makonda aliteuliwa kuwa Waziri wa wizara hiyo akichukua nafasi ya aliyekuwa Waziri Profesa Palamangamba Kabudi, ambapo awali alikuwa Naibu Waziri akisaidiana na Hamis Mwinjuma.
Makonda anachukua nafasi ya Kabudi ambaye ameteuliwa kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Ikulu (Kazi Maalumu).
Wakizungumza kwa nyakati tofauti, wadau wa soka walisema wanamshukuru Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kumteua Makonda kushika wizara hiyo kwani wanaamini atapambana kuipaisha sekta ya michezo kwa ujumla.
Kocha wa zamani wa Yanga na mchambuzi wa masuala ya michezo, Kennedy Mwaisabula ‘Mzazi’, alisema kuwa amefurahi kuona wizara hiyo imepata kiongozi kijana.
Alisema, Makonda ni mtu sahihi kwani anaamini kuwa atawaamsha waliolala kutokana na kauli zake huwa zimenyooka na anajua kutimiza majukumu yake.
“Niseme ukweli katika michezo kwa hivi sasa ameingia jembe, kwanza ni kijana, anaweza kukimbia hivyo ninaamini uwepo wa Makonda katika nafasi hiyo utachagiza maendeleo ya nchini.
“Ninampongeza Rais Dk. Samia kwa kumteua Makonda kwani kila mmoja aliona alivyokuwa akihamasisha wachezaji wa Taifa Stars walipokuwa wakishiriki michuano ya Mataifa Afrika (AFCON) na kufika hatua ya 16 bora,” alisema Mzazi.
Mchezaji wa zamani wa Yanga na Taifa Stars, Bakari Malima alisema kuwa kwanza anampongeza Rais Dk. Samia kwa uteuzi huo, kwani Makonda ni mwanamichezo kindakindaki, hivyo anaamini ataleta maendeleo katika michezo kwa ujumla.
Malima alisema kuwa Makonda anajua mpira lakini pia kuna Waziri Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba ni mwanamichezo hivyo wakikaa meza moja watafanya jambo zuri la maendeleo na kuifikisha mbali sekta hiyo nchini.
“Sisi wanamichezo kilio chetu kimesikika na Rais Dk. Samia kwa kutuletea waziri anayependa michezo, Makonda akikaa meza moja na Dk. Mwigulu tutafikia malengo katika sekta ya michezo,” alisema.
Naye promota wa ngumi za kulipwa, Meja Selemani Semunyu alisema kuwa aliyetoka ni mtu na aliyeingia ni mtu kabisa, hivyo anaimani kutokana na ujana wake ataisaidia michezo ikiwemo kuipaisha sekta ya ngumi.
“Ombi letu kwake tunajua nguvu kubwa imewekwa katika soka, mchezo ambao ni pendwa kabisa, lakini tunaomba pia atazame katika ngumi ili kuwawezesha kuendelea kufanya vizuri ndani na nje ya nchi.
“Tumeona Rais Dk. Samia alivyoweka nguvu katika michezo yote ikiwemo ngumi kwa mabondia wanaoshinda mapambano ya kimataifa, tunaamini tutafika mbali kwa muda mfupi tofauti na tulivyotarajia,” alisema Meja Semunyu.
Promota huyo alisema kuwa kutokana na ujana aliokuwa nao anaimani kubwa ataweza kuhudhuria katika matamasha yote ya mchana na usiku.
Semunyu alisema anampongeza Rais Dk.Samia kwa uteuzi huo na wataendelea kushirikiana bega kwa bega na serikali ili kuendelea kukuza ngumi hapa nchini.




