Na MWANDISHI WETU
KUMALIZIKA kwa michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika 2025 juzi ni wazi ndiyo mwanzo wa maandalizi ya fainali za AFCON 2027 zitakazofanyika katika nchi za Tanzania, Kenya na Uganda.
Hatua hiyo imejiri baada ya nchi hizo tatu kutoka Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), kukabidhiwa bendera ya CAF ikiwa ishara ya kuwa mwenyeji rasmi wa fainali hizo za 36 Afrika.
Nchi hizo tatu zilikabidhiwa bendera hiyo katika Uwanja wa Prince Moulay Abdellah jijini Rabat, Morocco baada ya kumalizika kwa mchezo wa fainali kati ya Morocco na Senegal, ambapo Senegal ilishinda kwa bao 1-0.
Ndoto ya Tanzania, Kenya na Uganda kuandaa fainali hizo ilikamilika mwaka 2023 baada ya CAF kuridhia ombi hilo.
Nchi za Tanzania, Kenya na Uganda, ziliomba kuandaa AFCON kwa pamoja kupitia maombi yaliyopewa jina la ‘Pamoja Bid’, ambapo Kamati ya Utendaji ya CAF iliridhia maombi hayo na kuzipiga chini Botswana, Senegal na Misri ambazo nazo ziliomba kuwa mwenyeji. Algeria iliomba, lakini ilijiondoa juzi.
Hiyo ni mara ya kwanza kwa nchi kutoka Jumuiya ya Afrika Mashariki kuandaa fainali za AFCON katika historia ya soka la Afrika.
VIGEZO PAMOJA BID KUKUBALIWA
Moja ya vigezo vya CAF kwa nchi kuwa mwenyeji wa Afcon ni uwepo wa viwanja sita ambapo viwili viwe na uwezowa kuchukua kila kimoja watu 40,000, viwili kila kimoja watu 20,000 na pia viwanja viwili kila kimoja kiwe na uwezo wa kuchukua watu 15,000.
Timu ya maofisa kutoka CAF ilimaliza ukaguzi wa awali wa miundombinu kuona utayari wa nchi hizo katika kuandaa fainali za AFCON.
Katika ukaguzi huo kwa upande wa Tanzania, CAF ilikagua Uwanja wa Benjamin Mkapa, Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), Hospitali ya Taifa Muhimbili.
Aidha, upande wa Zanzibar, ujumbe huo wa CAF ulikagua Uwanja wa Amaan, Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume na Hospitali ya Mnazi Mmoja.
MAKONDA AKUTANA NA DK. MOTSEPE
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Christian Makonda, juzi alikutana na Rais wa CAF, Dk. Patrice Motsepe jijini Rabat, Morocco na kumkabidhi barua kutoka kwa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.
Pamoja na kukabidhi barua hiyo, Makonda aliyeongozana na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo na Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa amemhakikishia Dk. Motsepe kuwa Rais Samia yupo tayari wakati wote kushirikiana na CAF katika utekelezaji wa mipango mbalimbali ya maendeleo ya kandanda ikiwemo mashindano mbalimbali.
Amesema Tanzania imepiga hatua kubwa katika maandalizi ya kuwa wenyeji wa AFCON 2027 sambamba na Kenya na Uganda na kwamba imedhamiria kuonesha tofauti kubwa na mashindano yaliyopita.
Aidha, Makonda amemuomba Dk. Motsepe kuiangalia Tanzania kimkakati ili mipango inayowekwa na Serikali ipate mafanikio makubwa yanayotarajiwa.
Kwa upande wake Dk. Motsepe amemshukuru Rais Samia kwa kumuandikia barua na salamu zake za upendo na ushirikiano kwa CAF na amemhakikishia kuwa CAF ipo tayari kufanya kazi bega kwa bega na Tanzania ili kufikia maendeleo makubwa katika kandanda.
Motsepe ameelezea kufurahishwa na jitihada kubwa zilizofanywa na Rais Samia na Serikali anayoiongoza katika maendeleo ya mpira ikiwemo ujenzi wa miundombinu, kufanya mashindano ya CHAN 2024 kwa mafanikio makubwa na maandalizi mazuri yanayoendelea kuelekea AFCON 2027.
Alisema CAF itatuma timu ya wataalamu kwenda Tanzania kushirikiana na Serikali na wadau mbalimbali katika kukamilisha maandalizi makubwa ya AFCON 2027 ambayo yanatarajiwa kushirikisha nchi 28 badala ya 24.
Motsepe ameahidi kuja Tanzania hivi karibuni kujionea maandalizi mbalimbali ya AFCON 2027 na kukutana na viongozi kwa mazungumzo.




