Na AMINA KASHEBA
KOCHA Mkuu wa Simba,Steve Barker amepania kuhakikisha leo kikosi chake kinachukua pointi tatu mbele ya Mashujaa FC.
Timu ya Simba inatarajiwa kushuka dimbani leo katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Mashujaa utaofanyika katika Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo jijini Dar es Salaam.
Pambano hilo, limepangwa kuanza kupigwa saa 10:00 jioni.
Katika mechi hiyo, Simba anashuka dimbani ikiwa na kumbukumbu ya kutoka sare 1-1 na Mtibwa Sugar.
Timu ya Mashujaa nayo itaingia uwanjani ikiwa na kumbukumbu mbaya ya kupachikwa mabao 6-0 dhidi ya Yanga.
Akizungumza maandalizi ya mchezo huo, Barker alisema wamejipanga kucheza vizuri kwa sababu wanatambua wapinzani wao Mashujaa ni timu nzuri yenye ushindani mkubwa katika ligi hiyo.
“Malengo yetu msimu huu ni kushinda nak utwaa ubingwa, pia tunatambua Mashujaa wamejipanga kufanya vizuri, sisi tutapambana kupata ushindi na kuwapa furaha mashabiki wetu,” alisema.
Kocha huyo alisema kumekuwa na mabadiliko katika kikosi chake kitu ambacho kimeleta mageuzi makubwa.
“Kumekuwa na mabadiliko katika kikosi chetu kuna baadhi ya wachezaji wanaingia na kutoka, hivyo tumejipanga kufanya vizuri na kupata matokeo mazuri japokuwa mchezo utakuwa mgumu, alisema.
Hata hivyo, kocha huyo alikiri kuwepo kasoro kadhaa katika kikosi chake ambazo amezifanyia kazi.
Mchezaji, Daud Semfuko alisema wachezaji wako tayari kwa mchezo wa leo dhidi ya Mashujaa Fc na wanatambua umuhimu wa kushinda mechi hiyo.
“Wachezaji tumejipanga vizuri kushinda, tunatambua ni mechi muhimu hivyo tutazingatia yale maelekezo ya walimu wetu ili kufanya vizuri,”alisema.
Kocha wa Mashujaa FC, Salum Mayanga alisema wanatambua wanaenda kukutana na timu bora, lakini wachezaji wake wamejipanga kuhakikisha wanafanya vizuri na kupata ushindi.
“Baada ya mechi iliyopita tumerudi nyumbani na kufanya mazoezi kuondoa kasoro zilizojitokeza, tumepata vipindi vitatu na kufanya uboreshaji, lakini nitawakosa wachezaji watatu ambao wapo katika majeruhi,” alisema.
Kocha huyo alisema pambano hilo halitakuwa rahisi kwa sababu wanakutana na timu yenye ubora Tanzania na Afrika.
“Timu kubwa yenye mashabiki wengi kwetu tutaangalia ni namna gani tutacheza kwa utulivu bila kupata changamoto kutoka kwa mashabiki, pia ni timu yenye wachezaji wazuri wa ndani na kigeni tutaingia kwa kuwaheshimu,” alisema.
Kocha huyo alitoa wito kwa mashabiki wa Mashujaa kuja kwa wingi katika mchezo huo kwa lengo la kuwapa hamasa wachezaji wao kufanya vizuri katika mechi hiyo.
Mchezaji wa Mashujaa,Ismail Mgunda alisema wachezaji wamejiandaa kupata ushindi.
“Mchezo uliopita tulipoteza kwa mabao mengi lakini awamu hii tumejiandaa mechi itakuwa ngumu na ushindani, pia tumefanyia kazi kasoro zote na kuangalia namna ya kuruhusu mabao,” alisema.
Katika msimamo wa ligi, Simba ipo nafasi ya sita ikiwa na pointi 13, ameshuka dimbani mara sita wakati Mashujaa FC ipo nafasi ya nane na pointi 13 amecheza michezo 10.




