Na NASRA KITANA
PAMOJA na kupata ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Cosmopolitan, Kocha wa Yanga, Pedro Goncalves amesema amesikitishwa na uchache mabao machache yaliyopachikwa wavuni tofauti na nafasi walizotengeneza.
Yanga ilipata ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Cosmopolitan katika mchezo wa hatua ya 64 bora ya Kombe la Shirikisho (FA), uliochezwa Uwanja wa KMC, Dar es Salaam na kutinga hatua ya 32 bora ya mashindano hayo.
Akizungumza baada ya mchezo huo, Kocha Pedro alisema timu yake bado imeendelea kuwa na tatizo la safu ya ushambuliaji na anahitaji kufanya marekebisho ya haraka ili kufanya vizuri zaidi katika mechi zinazofuata.
Alisema malengo yake ni kuona Yanga inafunga mabao mengi katika kila mchezo, hivyo atakwenda kuboresha na kuwapa mazoezi maalumu washambuliaji wake ili waweze kufunga mabao mengi.
“Tumeshinda lakini sijafurahishwa na matokeo ambayo tumeyapata katika mchezo dhidi ya Cosmo, tumetengeneza nafasi nyingi na wachezaji wangu wameshindwa kuzitumia, hivyo ninahitaji kuboresha zaidi kikosi changu hasa nafasi ya ushambuliaji,” alisema Pedro.
Kocha huyo alisema kila mchezaji ana jukumu la kuipambania timu na kuhakikisha anatumia vyema nafasi anazozipata ili kuzibadilisha na kuwa mabao.
Pedro alisema anajivunia kikosi alichokuwa nacho kwani wachezaji wamekuwa wakionyesha kiwango kikubwa, lakini anahitaji kupata dawa ya washambuliaji wake ili kuzitumia nafasi wanazozipata kuwa mabao.
Hata hivyo, Pedro alizungumzia uwezo wa nyota wake mpya, Buba Jammeh ambaye alifunga mabao mawili katika mchezo huo kuwa ni mmoja wa wachezaji wenye kiwango cha hali ya juu na kwamba ataisaidia timu kufikia malengo.
“Namjua vizuri Buba, najua uwezo wake lakini kwa hivi sasa hayuko vizuri sana, yuko katika mchakato wa kurejea katika kiwango chake hivyo nina imani atakapokuwa vizuri ni msaada mkubwa katika timu,” alisema Pedro.
Kocha huyo alisema pamoja na kupata ushindi lakini amekubali kiwango cha wapinzani wa Cosmopolitan kwani waliwaonyesha ushindani mkubwa.
Naye Buba alisema pamoja na kushinda mchezo huo bado hajaonyesha makali yake, hivyo anaamini atawafurahisha mashabiki katika mechi zitakazofuata.
Alisema huo ni mchezo wake wa kwanza kuichezea Yanga, ana furaha kuona mashabiki na wapenzi wa timu hiyo wamempokea vyema.
“Nimefurahi kuona nimeweza kusadia timu yangu katika mchezo wangu wa kwanza ikiwemo kupokelewa vyema na mashabiki, nitafanya mengi zaidi katika mechi zitakazofuata,” alisema.
Yanga inatarajia kuifuata Namungo, katika mchezo utakaofanyika Februari 22, mwaka huu ugenini kabla ya kurejea nyumbani kupepetana na JKT Tannzania, Februari 25, mwaka huu.




