Dar es Salaam
NA EMMANUEL MOHAMED
KAMISHNA Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Yussuph Mwenda, amewaonya baadhi ya wamiliki wa bandari kavu (ICDs) wanaokwepa kodi ambapo amesisitiza hatua kali zitachukuliwa kwa wahusika.
Kauli hiyo aliitoa jana katika kikao kazi kati ya Kamishna Mkuu wa TRA na wamiliki wa bandari hizo kilichofanyika jijini Dar es Saalam.
Alisema baadhi ya ICDs zinachochea kuweka mazingira ya ukwepaji wa kodi, hivyo TRA itaendelea kuzichukulia hatua kali.
“Najua kuna ukwepaji kodi unaofanyika katika baadhi ya bandari hizo za nchi kavu, tuna ushahidi lakini niliwaambia kuwa tunaziwezesha bandari zote kavu ziweze kufanya kazi kwa ufanisi. Mtaanza kusema sisi hatuhusiki. Watumishi wetu wapo pale, ninajua kinachoendelea ,”alisema.
Kamishna huyo alisema kuna haja kuhakikisha TRA na wamiliki wa bandari hizo kushirikiana kufanya ICDs zinakuwa salama kwa maslahi ya umma.
“Kuna baadhi ya watu wanachagua ICDs kwa kudai kuwa wanazipenda kwa sababu fulani lakini hawazichagui kwasababu ya ufanisi bali kwa sababu zingine,”alisema.
Kamishna huyo aliwataka wamiliki wa bandari hizo kufanya kazi ya utoaji huduma ndani ya saa 24 ili kuongeza ufanisi katika eneo la usafirishaji wa mizigo.
“Katika kuhakikisha tunalifanyia kazi hilo, tutaleta rasilimali watu kutoka TRA hivyo lazima tuweke miundombinu ya kisasa ambayo itawezesha ufanyaji wa kazi wa saa 24,”alisema.
Alisema TRA itaendelea kuwapatia ushirikianao wamiliki wa bandari kavu ili wafanye kazi kwa ufanisi mkubwa.
Katika hatua nyingine, Kamishna Mwenda aliwaahidi wamiliki wa bandari hizo kuzifanyia kazi changamoto ambazo wameziwasilisha ikiwemo eneo la mifumo na utoaji wa leseni ya uendeshaji wa bandari kavu.
Naye, Kamishna wa Forodha na Ushuru wa Bidhaa, Juma Bakari, alisema uwepo wa bandari kavu zimetoa mchango mkubwa katika ukusanyaji mapato.
“Katika kipindi cha miezi sita iliyopita, Idara ya Forodha ilikuwa inajukumu la kukusanya sh. trilioni 6.8. Kwa muda wa miezi sita tumefanikiwa kukusanya sh. trilioni 6.9 na tumezidia kwa asilimai 101.2,”alisema.
Alisema kitengo cha huduma cha forodha, kilikusanya sh. trilioni 3.6 ikiwa na lengo la kukusanya sh. trilioni 3.55.
“Ukichukua lengo la forodha la sh. trilioni 6.8 ambalo kitengo kilikusanya sh. trilioni 3.5 maana yake asilimia 52 ya makusanyo kwa kipindi hicho cha miezi sita, kimechangiwa na wadau wa ICDs waliopo hapa,”alisema. Mwenyekiti wa Wamiliki wa Bandari Kavu (CIDAT) Meleckzedeck Shange, alisema wadau hao wanakumbwa na baadhi ya changamoto ikiwemo upakiaji mizigo.




