Na MWANDISHI WETU, Zanzibar
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, amewasisitiza waumini wa dini ya Kiislamu kuyaendeleza mambo mazuri waliyokuwa wakiyatekeleza mwezi wa Ramadhani.
Dk. Mwinyi aliyasema hayo alipojumuika na waumini wa dini ya kiislamu katika swala ya Ijumaa iliyofanyika Msikiti wa Maisara mjini Unguja.
Alisema Ramadhani ni kipindi cha kujifunza mema na kumalizika kwake, haipaswi kuwa sababu ya kurudi katika maovu, bali ni fursa ya kuendeleza maadili mema na kuzidi kumcha Mungu.
KIFO CHA IMAM
Katika hatua nyingine, Rais Mwinyi aliwapa pole waumini wa msikiti huo kufuatia kifo cha Imam wao, Sheikh Saleh Ameir kilichotokea juzi.
Pia, alitumia fursa hiyo kuwatakia wananchi wote heri na furaha katika kusherehekea sikukuu ya Eid el Fitri leo.
MAKAMU WA PILI WA RAIS
Wakati huohuo, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Alhaj Hemed Suleiman Abdulla, aliwataka wazazi na walezi kuhimizana kuwadhibiti watoto hasa kipindi cha sikukuu hiyo ya Eid.
Abdulla alisema hayo jana alipowasalimia waumini wa Masjid ya Rahmaan uliopo Mfenesini, Wilaya ya Magharibi “A“ baada ya swala ya Ijumaa.
Alisema kuwadhibiti watoto katika sikukuu ni jambo la lazima kwa kila mzazi kuwakinga na majanga ikiwemo udhalilishaji.
“Suala la ulinzi kwa watoto huanza na mzazi na kuwasisisiza wazazi na walezi kuwapeleka watoto sehemu ambazo ni salama,” alisisitiza.
Abdulla alisema wazazi wanapaswa kuwavalisha watoto nguo za heshima kuwajenga katika maadili mema pamoja na kuwakinga na vishawishi mbalimbali wakiwa katika matembezi.
Mbali na hilo, aliwasisitiza waumini wa dini ya kiislamu na Wazanzibari kwa ujumla, kuendelea kuiombea nchi pamoja na viongozi wakuu walete maendeleo na kuipigania amani na utulivu.




