Na AMINA KASHEBA
RAIS wa Shirikisho la Muziki Tanzania, Addo November amesema bila ya uwepo wa amani hakuna jambo lolote linafanyika hapa nchini.
Akizungumza Dar es Salaam, Rais huyo alisema kazi za muziki zinahitaji uwepo wa amani ambapo wasanii wanafanya kazi zao kutokana na ujio wa wadau.
“Amani ikitoweka katika nchi au kitongoji, inafanya wasanii kushindwa kufanya kazi zao kwa uhuru na uchumi unashuka kutokana kukosekana kwa mapato ya fedha.
“Amani ndiyo kitu cha muhimu katika taifa hivyo Watanzania wanapaswa kuendeleza tunu hii muhimu, kwani tunaona baadhi ya nchi ambazo hivi sasa zinavurugu, hakuna maendeleo.
“Tunapaswa kudumisha hii amani kwa sababu ikipotea inakuwa ngumu kuirudisha, pia serikali yetu chini ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan inapambana kuhakikisha taifa linakuwa katika hali tulivu,” alisema November.
Rais huyo aliongeza kuwa mbali ya wasanii kufanya kazi zao za muziki, bado ataendelea kuunga mkono juhudi za serikalik uhakikisha michezo inakuwa chanzo kikubwa cha kutengeneza ajira kwa vijana.
“Tunapaswa kuendeleza amani ya nchi yetu na kuwa mabalozi wakubwa hivi sasa tunatakiwa kushikamana maana Tanzania yetu inasifika kwa upendo na amani,” alisema November.




