Na AMINA KASHEBA
SERIKALI imeendelea kuonesha dhamira yake ya dhati katika kuhakikisha mashindano ya AFCON 2027 yanafanyika kwa mafanikio makubwa, baada ya kueleza milango ipo wazi kupokea maoni.
Hatua hiyo, imekuja baada ya serikali kulipa ada ya ushiriki ya shilingi bilioni 76, hatua inayodhihirisha uzito wa maandalizi hayo.
Akizungumza jijini Dar es Salaam, katika mkutano na wadau wa michezo, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Gerson Msigwa alisema wizara ipo tayari kupokea maoni kutoka kwa wadau mbalimbali.
Alisema lengo la kufanya hivyo ni kuhakikisha mashindano hayo yanaacha historia chanya na yenye mafanikio makubwa kwa nchi.
“Milango ipo wazi kwa kila mtu kutoa mawazo yake. Kila mmoja anapaswa kutumia nafasi aliyonayo kuchangia mafanikio ya AFCON 2027. Lengo letu ni kuona Tanzania ikiweka rekodi nzuri na kujivunia mafanikio haya,” alisema.
Katibu huyo alifafanua kuwa mashindano ya AFCON 2027 yanatarajiwa kuwa chachu ya maendeleo katika sekta mbalimbali zikiwemo utalii, biashara na ajira.
“Hii ni fursa kwa Tanzania kuonesha utamaduni wake na ukarimu kwa wageni watakaokuja kutoka sehemu mbalimbali za dunia,”alisema Katibu huyo.
Msigwa aliwaomba Watanzania kuchangamkia fursa hiyo kwa ubunifu na uzalishaji wa bidhaa na huduma zitakazowapa furaha na kumbukumbu nzuri wageni watakaotembelea nchi wakati wa mashindano hayo.
“Tunawahimiza Watanzania kutumia nafasi hii vizuri kwa kubuni na kuandaa vitu vitakavyowavutia wageni wetu. Hii ni fursa ya kipekee kwa taifa kujitangaza kimataifa,” alisema.
Katibu huyo aliongeza kuwa serikali imeendelea kuonesha dhamira yake ya dhati katika kuhakikisha mashindano yanafanyika kwa mafanikio makubwa.
“Baada ya kuwekeza fedha nyingi katika maandalizi ya tukio hilo kubwa la kimataifa, bado Watanzania wanatakiwa kuitumia vizuri kukuza uchumi wao na nchi kwa ujumla,” alisema.
Msigwa alisema kuwa serikali tayari imelipa ada ya ushiriki ya shilingi bilioni 76, hatua inayodhihirisha uzito wa maandalizi hayo.
Alisema kuwa uwekezaji huo ni sehemu ya mkakati kuhakikisha Tanzania inaandaa mashindano ya kiwango cha juu yatakayovutia wageni kutoka mataifa mbalimbali barani Afrika na duniani kwa ujumla.
“Serikali imejipanga na imetoa fedha nyingi kuhakakikisha mashindano haya yanafanyika kwa kiwango kikubwa, pia imelipa ada ya ushiriki shilingi bilioni 76, “alisema.




