Na SIMON NYALOBI
JAJI Mkuu Mstaafu, Profesa Ibrahim Juma, ametaja mambo matatu makubwa kuhusu Tume ya Kuchunguza Matukio ya kabla na baada ya Uchaguzi Mkuu Oktoba 29, 2025.
Amesema kuundwa kwa tume hiyo kumeipa sifa kubwa Tanzania kimataifa.
Profesa Juma, mmoja wa majaji wakuu wastaafu aliyesimamia kwa dhati mfumo wa mahakama nchini, alitoa uchambuzi huo, jijini Dar e Salaam, alipozungumza na vyombo vya habari.
MAMBO MATATU
Kwa mujibu wa Profesa Juma ambaye ni mjumbe wa tume hiyo, kuundwa kwa tume hiyo ni heshima kubwa kwa nchi kwani inaheshimika kutokana na kushughulikia changamoto zake.
“Kwa hiyo kuwa na tume hii, nchi inaonyesha kwamba tuna uwezo mkubwa wa kushughulikia masuala makubwa kama hayo, na kwamba tunafanya kazi zetu kwa uwazi zaidi, kwamba tuna taasisi zinaweza kufanya hizo kazi.
Profesa Juma, alifafanua zaidi: “Na taarifa yetu inatakiwa vilevile ikidhi hayo matarajio makubwa ambayo yanayotokana na hiyo Tume, kwa hiyo taswira kubwa ambayo naiona hapa ni namna gani tunaiambia dunia kwamba tuna uwezo wa kushughulikia changamoto zetu na kuzitafutia ufumbuzi,” alisema.
Profesa Juma alifafanua sifa ya pili ya Tume, akiema ina watu wabobezi katika fani mbalimbali akitoa mfano wa Mwenyekiti wake, Jaji Mkuu Mstaafu Othman Chande, ambaye ana sifa kutokana na kuwa mjumbe katika kamati lukuki za kimataifa.
Alisema Jaji Chande amekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Kuchunguza kifo cha Katibu Mkuu mstaafu wa Umoja wa Mataifa (UN), Dag Hammarskjöld na matukio ya Sudan katika Jimbo la El Fasher.
Alisema Jaji Mkuu mstaafu Chande, aliwaelekeza wajumbe wa tume hiyo kwamba, ripoti yao izingatie viwango vya kimataifa, hivyo wasiegemee sheria za Tanzania pekee bali waangalie na sheria za kimataifa.
Pia, alisema wasifu wa wataalamu wa video na uhalifu wa mitandaoni wana sifa za kimataifa wakifanya kazi katika nchi za Afrika Kusini na Uingereza.
Uhuru wa Tume, alitaja jambo la tatu ni kuhusu uchukuaji wa taarifa za matukio, akisema Tume hiyo imetembelea maeneo yote yaliyokumbwa na vurugu na kuzungumza na majeruhi, wafiwa na waliopotelewa na ndugu zao ambao wote wameleta ushahidi wao.
MUFTI
Kwa upande wake Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Dk. Abubakar Zubeir, alisema ana matumaini na matarajio makubwa na Tume hiyo kutokana na kuwa na wajumbe wenye weledi mkubwa wa kutekeleza kazi hiyo.
Dk. Zubeir alisema hayo juzi, alipotoa maoni yake kuhusiana na matarajio yake kwa Tume hiyo iliyoundwa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.
“Tume naona ina weledi mkubwa na ina uwezo mkubwa na umahiri mkubwa, kwa sababu hata mimi mwenyewe nimeitwa kwenda kujaribu kuangalia maoni yangu au rai yangu, kwa hiyo nimeona kwamba ina uwezo mkubwa.
“Na yaliyotokea kabla na yatakayokuja baadaye na hali halisi naona Tume inaweza ikafanya kazi nzuri sana, nina hakika kwamba mpaka sasa hivi imefanya kazi moja nzuri sana, kwa hiyo tume itatuweka mahali pazuri sana,”alisema.
Dk. Zubeir alimpongeza Rais Dk. Samia, kwa wazo na fikra nzuri kwa kuunda Tume hiyo kubwa ya kuanzisha tume hiyo.
TUME
Tume hiyo iliongezewa muda hadi Aprili 24,mwaka huu kukamilisha kazi yake kwa ufanisi.
Kulingana na Tume hiyo, sababu za kuomba kuongezewa muda ni pamoja na kuiwezesha kukamilisha uchambuzi wa Ushahidi, taarifa na maoni yaliyopokelewa.
Sababu nyingine, ni kutoa fursa kwa wataalamu wa uchunguzi wa kisanyansi kufanyia kazi baadhi ya vielelezo vipya vilivyowasilishwa.
Tayari jumuiya ya kimataifa likiwemo Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa (UNHC), kupitia Kamishna wake, Volker Turk na Jumuiya ya Madola kupitia Mjumbe Maalumu wa Sekretarieti yake, Rais mstaafu wa Malawi, Lazarus Chakwera, wameisifu Tanzania kwa kuunda Tume hiyo.



