Na NASRA KITANA
YANGA leo itakuwa dimbani kusukuma kete yake muhimu dhidi ya JS Kabylie ya Algeria, kujiweka nafasi nzuri zaidi katika mbio za kuwania kutinga robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika (CAFCL).
Timu hiyo yenye maskani yake mtaa wa Twiga na Jangwani jijini Dar es Salaam, itachuana na Kabylie katika mechi ya pili ya kundi B la michuano hiyo itakayopigwa Uwanja wa Hocine Ait Ahmed, Tizi Ouzou nchini Algeria.
Katika mtanange huo utakaoanza saa 1:00 usiku, Yanga inahitaji ushindi au sare ya aina yoyote kuweka sawa hesabu zake katika safari ya kutinga robo fainali kufuatia mechi ya kwanza dhidi ya AS Far Rabat ya Morocco, kushinda bao 1-0 nyumbani.
Akizungumzia mechi hiyo, Kocha wa Yanga, Pedro Goncalves, amesema ameiandaa vyema timu yake kuhakikisha inapata ushindi katika mtanange huo.
Pedro timu yake ipo vizuri na ina nafasi ya kupata ushindi.
Amesema anajua utakuwa mchezo mgumu lakini hawatakubali kuona wanapoteza.
“Tumefanya mazoezi ya kutosha kuelekea katika mchezo huo, lengo letu kubwa ni kupata ushindi na kusonga mbele, tunajua utakuwa mchezo mgumu lakini hatutakubali kurejea bila ya pointi tatu muhimu,” amesema Pedro.
Naye nahodha wa timu hiyo, Bakari Mwanyeto alisema wachezaji wamejipanga vyema kuhakikisha wanapata ushindi katika mchezo huo.
“Ujue tunaingia katika mchezo mgumu, sisi kama wachezaji tumekaa kwa pamoja na kuelekezana kuhakikisha tunapata ushindi,” amesema Mwanyeto.
Katika kundi B, Yanga ipo pamoja na timu za Al Ahly ya Misri, AS FAR ya Morocco na JS Kabylie ya Algeria.




