Na MWANDISHI WETU
SERIKALI imesema ujenzi wa Uwanja wa soka wa kisasa jijini Dodoma, unaendelea kwa kasi na hivi sasa umefikia asilimia 2.7.
Hatua hiyo ni sehemu ya ahadi za Rais Dk. Samia Suluhu Hassan ambaye ameahidi ndani ya siku 100 baada ya kuapishwa kuongoza nchi katika kipindi cha pili cha uongozi wa Serikali ya Awamu ya Sita anayoiongoza.
Rais Dk. Samia aliahidi hayo katika mikutano mbalimbali ya kampeni za Uchaguzi Mkuu, kati ya Agosti na Oktoba mwaka huu.
Akizungumza Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa amesema, kazi ya ujenzi wa Uwanja wa michezo Dodoma imeanza na hivi sasa umefikia asilimia 2.7.
Msigwa alisema hayo wakati wa kikao kazi na kampuni inayojenga uwanja huo ya LIMONTA kutoka nchini Italia ambapo alisisitiza kazi ya ujenzi imechelewa kuanza kutokana na kuhamishwa kwa eneo la ujenzi lililopangwa awali.
Vilevile, Msigwa alitoa maagizo kwa mkandarasi huyo kuongeza mitambo ya kufanyia kazi, watumishi na wataalamu ambao ni wazawa ili kuwezesha vijana kupata ajira sambamba na kupata ujuzi zaidi kwa wazawa hao.
“Mpaka hivi sasa kuna jumla ya wakandarasi 34 ambapo 27 ni Watanzania na wanaendelea kufanya kazi na wengine wataendelea kuajiriwa.
“Lengo ni kuhakikisha Watanzania wanapata ajira kwa wingi kupitia ujenzi wa miundombinu ya michezo nchini,” alisema Msigwa.
Katika hatua nyingine, Msigwa amemtaka mkandarasi huyo kukamilisha kazi kwa wakati ambayo itakua na hadhi ya makao makuu ya nchi.
Alisema kwa upande wa Uwanja wa Arusha, ujenzi unakwenda vizuri ambapo hivi sasa umeshafikia asilimia zaidi ya 70.
“Katika ujenzi wa Uwanja wa Arusha, hivi sasa umefikia zaidi ya asilimia 70 ambapo mkandarasi anaendelea na ujenzi kwa kasi, tunaamini ujenzi wa viwanja vyote utakamilika kwa wakati kabla ya kuanza kwa michuano ya Mataifa ya Afrika (AFCON 2027), ambapo Tanzania tutakuwa wenyeji tukishirikiana na Kenya na Uganda,” alisema Msigwa.
Naye Mwakilishi wa kampuni ya LIMONTA Angelo Redolfi, ameahidi kufanya kazi hiyo kwa bidii na uwazi kwa kuzingatia maelekezo ya serikali ili kukamilisha uwanja wenye viwango bora vinavyotakiwa.
“Ninaahidi kufanya kazi kwa bidii na uwazi kwa kuzingatia maelekezo ya serikali ili kukamilisha uwanja wenye viwango bora vinavyotakiwa,” alisema.




