Na MWANDISHI WETU
KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dk. Asha-Rose Migiro, amesema uimara wa CCM unatokana na wanachama wake kujitokeza kikamilifu katika mikutano ya chama kwa kuwashirikisha wanachama wa CCM pamoja na wananchi wasiokuwa wanachama, hali inayokifanya chama hicho kuendelea kuwa imara na chenye mvuto kwa Watanzania.
Akizungumza na mabalozi wa mashina na wanachama wa CCM katika ukumbi wa Diamond Jubilee, Wilaya ya Ilala mkoani Dar es Salaam, Dk. Migiro amesema ubora wa CCM unatokana na siasa zake za kujenga hoja na kuimarisha imani ya kudumu kwa wananchi, akisisitiza kuwa misingi hiyo imeifanya CCM kuwa chama chenye uthabiti wa kisiasa kwa miaka mingi.
Ameeleza kuwa chama kimeweka utaratibu madhubuti wa kuimarisha vikao vya mashina kwa kukutana mara kwa mara, akibainisha kuwa mikutano hiyo ni nyenzo muhimu ya kusikiliza wananchi, kujenga mshikamano na kuimarisha demokrasia ya ndani ya chama.
Dk. Migiro amesisitiza kuwa itikadi ya CCM itaendelea kujengwa juu ya misingi ya utu, ujamaa na kujitegemea kama inavyobainishwa kwenye kauli mbiu ya chama “Kazi na Utu, Tunasonga Mbele”, akieleza kuwa dhamira ya CCM ya kushika Dola inalenga kujenga utu wa Mtanzania kwa kuboresha maisha yao kupitia ujenzi wa miundombinu, hospitali na huduma nyingine za kijamii.
Akifafanua nafasi ya mashina ndani ya chama, alisema licha ya kuonekana kama ngazi ndogo ya uongozi, mashina ndiyo nguzo kuu inayobeba uimara na umadhubuti wa CCM. “Mashina ni moyo wa Chama Cha Mapinduzi,” amesisitiza.
Aidha, ametoa wito kwa wanachama kushiriki kikamilifu katika vikao vya mashina na kuendelea kutangaza maendeleo yanayopatikana chini ya uongozi wa CCM, huku akiwataka mabalozi kuenzi alama za chama, kuendesha mikutano kwa nidhamu na kuwashirikisha wananchi katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo.




