MIAMI, Marekani
BAADA ya kupita miaka 11, bondia Manny Pacquiao kutoka Ufilipino na Mmarekani Floyd Mayweather , wamekubali kuzichapa tena katika pambano la kulipwa litakalopigwa Septemba 19, mwaka huu.
Pacquiao, 47 na Mayweather ,48, wanatarajiwa kuzichapa katika Ukumbi wa Sphere uliopo Las Vegas nchini Marekani huku pambano likitarajiwa kuwa mubashara kupitia Netflix.
Mayweather ambaye ni bingwa wa zamani wa dunia alitangaza kama atarejea ulingoni wiki iliyopita.
Pambano hilo litakuwa la kwanza kwa Mmarekani huyo tangu mwaka 2017, aliposhinda kwa TKO dhidi ya Conor McGregor.
Kwa upande wa Pacquiao alistaafu masumbwi mwaka 2021 kabla ya kurejea Julai mwaka jana alitoka suluhu dhidi ya Mario Barrios katika pambano la ubingwa wa WBC uzito wa welter.
Mara ya kwanza, Mayweather na Pacquiao walizichapa mwaka 2015 katika pambano lililopewa jina la ‘Pambano la Karne’.
Katika pambano hilo lililofanyika Las Vegas, Mayweather alimpiga Pacquiao kwa pointi.
Wakati Mayweather akishinda mapambano yote 50 aliyopigana katika historia yake, Pacquiao, ameshinda 62 kati ya 73.




