Na MWANDISHI WETU
YANGA imetuma salamu kwa watani wao jadi Simba, baada ya kuinyanyasa JKT Tanzania kwa kuifunga 5-0 katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara uliopigwa Uwanja wa KMC Complex jijini Dar es Salaam.
Ushindi huo ni salamu tosha kwa Wekundu wa Msimbani kueleka katika mchezo wa ‘dabi’ utakaochezwa Machi Mosi, mwaka huu katika Uwanja wa New Amaani Complex, Zanzibar.
Baada ya matokeo hayo, Yanga inaongoza ligi hiyo ikiwa na alama 28, ikiishusha JKT Tanzania hadi nafasi ya pili katika msimamo kwa tofauti ya mabao ya kufunga na kufungwa.
Yanga imecheza mechi 10 na JKT Tanzania imeshuka dimbani mara 17 na ina poin ti 28 katika ligi hiyo yenye ushindani mkubwa.
Mchezo ulianza kwa kasi huku timu zote zikipambana kusaka ushindi lakini dakika ya sita, Mohamed Hussein ‘Tshabalala alifunga bao la kuongoza kwa shuti, baada ya kumalizia pasi safi kutoka kwa Dube Abuya.
Mpira uliendelea kwa kasi na dakika ya 20 kipa wa JKT , Ramadhan Chalamanda alifanya kazi ya ziada kupangua shuti la Israel Mwenda, baada ya kupokea pasi nzuri kutoka kwa Mudathir Yahya.
JKT Tanzania walikosa bao, dakika ya 41 ya mchezo huo kupitia kwa mchezaji wake, Paul Peter ambaye alifumua shuti lililotoka nje ya lango la Yanga.
Dakika ya 60, Yanga ilipata bao la pili kupitia kwa Laurindo Aurelio ‘Dupe’ baada ya kupiga mpira kwa kichwa kufuatia kupokea pasi kutoka kwa Israel Mwenda.
Kabla hawajamaliza kushangilia dakika ya 62, Mudathir Yahya alipachika bao la tatu baada ya kupiga shuti kali lililokwenda wavuni moja kwa moja, Mudathir alimalizia mpira uliogongwa mwamba ambao ulipigwa na Prince Dube.
Prince Dube katika dakika ya 85 alifunga bao la nne kwa shuti na dakika ya 89, Yanga ilipata bao la tano kupitia kwa Shekhani Khamis.
Yanga iliwakilishwa na Djigui Diarra, Ibrahim Abdulla, Dikson Job, Maxi Nzengeli, Mudathir Yahya, Israel Mwenda, Allan Okello, Mohamed Hussein, Laurindo Dilson/Mwanengo, Prince Dube na Duke Abuya/.
JKT Tanzania: Ramadhani Chalamanda, Anuary Kilemile, Karimu Mfaume, Hassan Nassor, Sospeter Bajana, Salehe Karabaka, Edson Katanga, Ally Msengi, Pascal Mussa, Paul Peter na Mohemed Bakari.




