Na MWANDISHI WETU
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan, amemuasili mtoto mchanga wa kike leo tarehe 11 Machi, 2026, katika makazi yake, Ikulu Chamwino, jijini Dodoma.
Mtoto huyo aliyepewa jina la Grace Samia Suluhu, alitelekezwa mjini Nzega, mkoani Tabora, amekabidhiwa kwa Rais Dk. Samia.
Akizungumza wakati wa kukabidhi mtoto huyo, Mkuu wa Wilaya ya Nzega, Naitapwaki Tukai, amesema mtoto huyo aliokotwa Januari 17, 2026 akiwa ametelekezwa katika jirani na nyumba ya wageni ya Kasulu, Nzega mjini.
Amesema alipopata taarifa hizo alishirikiana na jeshi la polisi kumchukua na kumpeleka hospitalini kwa uchunguzi na uangalizi, huku juhudi za kumtafuta mama yake zikiendelea bila mafanikio.
Rais Dk. Samia amemkaribisha mtoto huyo katika familia yake na kuahidi kumpa malezi, ulinzi na huduma zote muhimu ili akue katika mazingira salama na yenye upendo.
“Wanaotupa watoto hawajui wanalolifanya. Kuliko kumtupa mtoto ni afadhali ukamkabidhi katika mamlaka za kisheria au kituo cha kulelea watoto. Kila mtoto aliyezaliwa ni hazina na hatuijui kesho yake,” amesema Rais Dk. Samia.




