Na MWANDISHI WETU
WATANZANIA Saba waliokuwa nchini Iran wamewasili nchini leo Machi 13, 2026, kufuatia operesheni ya uokozi iliyoratibiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Watanzania hao wamewasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) saa 8:40 usiku kwa kutumia Shirika la Ndege la Uturuki, wakitokea nchini Uturuki ambako walipokelewa awali baada ya kuvuka mpaka wa nchi kavu wakitokea nchini Iran.
Watanzania hao wamepokelewa na Mkurugenzi wa Idara ya Mashariki ya Kati kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Abdallah Kilima, pamoja na maafisa wengine wa wizara.
Mapokezi ya Watanzania hao yaligubikwa na hisia za faraja kutoka kwa ndugu na jamaa waliokuwa wakihofia usalama wa wapendwa wao.
Wakizungumza baada ya kuwasili uwanjani hapo, Watanzania hao wameishukuru serikali kwa kuratibu zoezi la kurejeshwa kwao nchini.
Serikali ya Tanzania ilichukua hatua za dharura kulinda maisha ya raia wake waliokuwa nchini humo kwa masomo na shughuli nyingine.
Safari ya kurejea nyumbani kwa Watanzania hao ilianzia kwenye mpaka wa Razi (Iran) na kufika Kapıkule (Uturuki) mnamo Machi 11, 2026 na kupokelewa na Balozi wa Tanzania nchini Uturuki, Iddi Seif Bakari na Maafisa wa Ubalozi wa Tanzania.




