ABDUL DUNIA Na ZIANA BAKARI
IKIWA ni siku nne tangu kipa wa Yanga, Djigui Diarra kufungiwa mechi tatu, adhabu hiyo inaweza kubadili taswira katika vita ya kuwania tuzo ya kipa bora wa Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu.
Diarra alifungiwa mechi hizo na Bodi ya Ligi Kuu Tanzania Bara (TPLB) Ijumaa iliyopita, kufuatia mlinda lango huyo raia wa Mali kufanya kosa la kumshambulia mwamuzi wa kati wa mechi dhidi ya Mtibwa Sugar baada ya mtanange huo kumalizika katika Uwanja wa Jamhuri, Dodoma.
Kutokana na adhabu hiyo, Diarra anatarajiwa kukosa mechi dhidi ya Tanzania Prisons, Pamba Jiji na Mbeya City.
Hatua ya kipa huyo kukosa mechi tatu zijazo za Yanga, inaweza kuwarudisha mchezoni makipa mbalimbali na kuongeza ushindani katika vita ya kipa bora wa Ligi Kuu msimu huu.
Kwa mujibu wa kanuni, tuzo ya kipa bora inakwenda kwa mlinda lango ambaye hajaruhusu bao katika mechi nyingi zaidi.
Katika ligi hiyo, Diarra ndiye kinara akiwa amecheza mechi 10 bila ya kuruhusu bao huku akifuatiwa na Aishi Manula wa Azam FC (6), Erick Johora wa Mashujaa (6), Jean Noel wa TRA United (6).
Wengine ni Djibrilla Kassali wa Simba (5), Zuberi Foba wa Azam FC (5), Yona Amosi kutoka Pamba Jiji (5), Ally Salim wa Dodoma Jiji (5) na Mussa Mbisa wa Tanzania Prisons (5).
Kama makipa hao watacheza vizuri katika mechi tatu zijazo na kutoruhusu bao ni wazi ushindani mpya utazaliwa katika mbio za kuwania tuzo ya kipa bora wa michuano hiyo msimu huu.
Kocha wa Buguruni Youth, Omary Mbweze alisema mechi tatu ni nyingi kwa kipa hivyo adhabu hiyo inaweza kumgharimu kwa kuwa wenzake wanaweza kufanya vyema zaidi na yeye akakosa ufiti wa mechi atakaporejea dimbani.
“Kukosa mechi tatu ni pigo, inaweza kusababisha kukosa utimamu katika mechi hivyo ubora wake, unaweza kupungua,” Mbweze.
Kocha wa Mbeya City, Mecky Maxime, alisema haoni sababu ya kipa huyo kumuathiri kwa kuwa atapata muda mwingi zaidi wa kujipanga ili kuwa bora zaidi.
“Kukosa mechi tatu ni jambo la kawaida na nafikiri atapata muda wa kupumzika zaidi, lakini ni suala la kawaida katika mpira,” alisema Mexime.
Mbali na kufungiwa mechi tatu, pia Diarra ametakiwa kulipa sh. milioni nne kwa makosa mawili tofauti ambapo kila kosa linagharimu faini ya sh. milioni mbili.




