Na NASRA KITANA
RAIS wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania(TFF), Wallace Karia amewataka wanamichezo nchini, kuhakikisha wanaendelea kudumisha amani kwani ndiyo nguzo ya kufanya vizuri katika mashindano mbalimbali.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi jijini Dar es Salaam, Karia amesema kuwa amani na mashikamano kwa nchi inasaidia kuendeleza michezo nchini na kupata burudani pale wanapoenda viwanjani.
“Amani katika kila jambo ndio msingi katika kila kitu, hivyo sis Watanzania tunatakiwa kuhakikisha kwamba amani inalindwa ili michezo ifanyike na kukuza soka letu na kuongeza pato la taifa kupitia michezo,” amesema.
Karia amesema amani ni nguzo ya taifa na alama ya Mtanzania kwani taifa hili ni nchi ambayo imejenga umoja,upendo na mshikamano.
“Napenda kuwahamasisha wadau wa michezo, kuimarisha amani na mshikamano, pia nawaomba vijana wote kushiriki michezo kwani michezo kwa sasa ni burudani, afya na ajira ndio maana Rais Dk. Samia Suluhu Hassani amewekeza fedha nyingi katika sekta ya michezo,” alisema Karia.
Karia alisema Tanzania imeweza kushiriki katika michezo, ndani na nje ya nchi sababu ni nchi yenye amani hivyo, kila mmoja anatakiwa kulinda na kuitunza amani ya nchi.




