Na NASRA KITANA
KOCHA wa Yanga, Pedro Goncalves, amesema wamejipanga vizuri kuhakikisha wanapata ushindi katika mchezo dhidi ya Mbeya City leo, kujiweka nafasi nzuri kutimiza malengo waliyojiwekea.
Yanga itashuka dimbani kumenyana na Mbeya City saa 12:30 jioni katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara utakaochezwa Uwanja wa KMC, Dar es Salaam.
Akizungumza Dar es Salaam, Pedro alisema wanaiheshimu Mbeya City kutokana na ubora wake lakini hawatakubali kupoteza mechi hiyo.
Pedro alisema amepata muda wa kufanya maandalizi na kurekebisha mapungufu yaliyojitokeza katika mchezo uliopita kufanya vizuri katika mchezo huo muhimu.
“Tumejipanga vizuri kuhakikisha tunapata ushindi, kila mchezo kwetu ni fainali, tunahitaji kupata pointi tatu muhimu kusalia kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu,” alisema.
Kocha huyo alisema wachezaji wake wapo vizuri isipokuwa wataendelea kumkosa straika Prince Dube na Laurindo Aurelio ‘Depu’ ambao bado ni majeruhi.
Kocha wa Mbeya City, Mecky Mexime, alisema anajua mchezo utakuwa mgumu lakini wataingia katika mtanange huo bila ya kuihofia Yanga.
Alisema ni mchezo mgumu watacheza kwa akili na kuwaheshimu wapinzani wao lakini wao pia wanamitego yao kuhakikisha wanapata matokeo mazuri.
Mexime aliwataka mashabiki na wapenzi wa timu hiyo kujaa kwa wingi uwanjani kuwapa sapoti na kuangalia timu yao jinsi ilivyobadilika kwa sasa.
Mchezaji wa Mbeya City Sudi Dondola, alisema kila mchezaji amejipanga vizuri kuhakikisha wanapambana na Yanga kupata ushindi.
Katika msimamo wa Ligi Kuu, Yanga ipo kileleni ikiwa na pointi 44 huku Mbeya City ikishika nafasi ya 12 kwa pointi 17, kila moja ikishuka dimbani mara 18.




