Na VICTOR MKUMBO
MWANARIADHA mkongwe na kocha wa mchezo huo, Suleiman Nyambui, amesema michezo na utamaduni kwa ujumla ina nafasi kubwa ya kutunza na kuendeleza amani iliyopo nchini.
Akizungumza jijini Dar es Salaam, Nyambui alisema michezo na utamaduni ina sehemu kubwa ya kudumisha amani kwani inakutanisha watu wengi na wa matabaka tofauti kwa wakati mmoja.
“Hata katika kamati ya michuano ya Olimpiki, huwa hawachagui matabaka na badala yake mashindano hayo hushirikisha nchi zote bila kujali itikati,” alisema.
Alifafanua kuwa kwa Tanzania michezo yote ikiwemo ngoma za asili zina nafasi ya kipekee katika kuimarisha amani kwa kuwafanya watu kufurahi kwa pamoja.
”Michezo ina nafasi kubwa katika kudumisha amani na umoja uliyopo nchini.
” Pia burudani husaidia kuwaweka wadau sehemu moja na kufurahia ngoma zikiwemo za asili, kitu ambacho kimekuwa utamaduni wa Watanzania kwa miaka mingi,” alisema Nyambui.
Nyambui alisisitiza kwamba, serikali bado ina nafasi ya kuanzisha mashindano ya michezo na burudani kuanzia ngazi za awali ,kuhakikisha watu wote wanapata muda wa kuburudika.
Alisema kurejeshwa kwa mashindano hayo, kutawafanya vijana kujikita katika utamaduni zaidi na kuachana na mambo ya makundi yasiyofaa kwa jamii.
”Tusisubiri hadi viongozi waseme wana shughuli fulani ndipo tuanze kutafuta wacheza ngoma, wanatakiwa kuandaliwa kwa mashindano kuanzia ngazi za awali kuhakikisha wanapatikana washindi wa kitaifa.
”Hii pia itasaidia kupunguza au kumaliza vijana ambao wanaingia katika makundi yasiyofaa kwa jamii,” alisema Nyambui.




