Na MWANDISHI WETU
DAKTARI Bingwa wa Maradhi ya Moyo wa Hospitali ya Shifaa ya Kinondoni, jijini Dar es Salaam, Lulu Mageta, amesema vijana wengi hukumbwa na tatizo la shinikizo la damu kwa sababu hawana kawaida ya kupima afya zao mara kwa mara.
Dk. Lulu ametaja baadhi ya dalili za ugonjwa huo kuwa ni maumivu chini ya moyo, kuchoka kusikokuwa kwa kawaida na mapigo ya moyo kwenda haraka.
“Ukiona unatembea umbali mdogo tu unachoka sana, umbali ambao zamani ulikuwa unatembea bila shida, basi ujue umeanza kupata shinikizo la damu na ugonjwa huu hauji ghafla kama baadhi yetu tunavyodhani, unachukua muda mrefu ndiyo maana tunashauri kupima mara kwa mara,” alisema.
Amewataka vijana kupima afya zao mara kwa mara, kwa sababu idadi kubwa kwa sasa wanasumbuliwa na maradhi hayo.
Dk. Lului amesema zamani, ugonjwa huo, ulizoeleka kuwasumbua watu wenye umri mkubwa ambao walikuwa katika hatari ya kupata maradhi, lakini kwa sasa vijana wengi wenye miaka chini ya miaka 40, wanapata tatizo hilo.
Dk. Lulu, aliyasema hayo jana jijini Dar es Salaam, wakati akizungumzia ongezeko la magonjwa ya moyo hasa kwa vijana walio chini ya miaka 40.
Alisema vijana wanatakiwa kuwa na utaratibu wa kupima afya ya moyo mara kwa mara, kujua afya zao badala ya kusubiri mpaka hali inapokuwa mbaya, ndiyo wafanye hivyo wanapofika hospitali.
“Zamani ilionekana kuwa maradhi ya shinikizo la damu, yanawashambulia watu wazima sana pekee, lakini kutokana na kubadilika kwa mtindo wa maisha, watu wengi hawafanyi mazoezi kwa hiyo, vijana wengi kwa sasa wanasumbuliwa na shida kama hiyo,” alisema Dk. Lulu.
Aliongeza: “Tusiendelee kuwa na mawazo yale yale ya zamani kwamba shinikizo la damu ni kwa wazee kwa sababu vijana wengi wanakufa ghafla kutokanana magonjwa haya, tubadili mtindo wa maisha ,tufanye mazoezi,” alisema
Aidha, alisema zamani haikuwa rahisi kumkuta kijana wa chini ya miaka 40 akisumbuliwa na maradhi ya moyo, miaka ya hivi karibuni, imekuwa kawaida kabisa kuwaona watu wa rika hilo wakisumbuliwa na moyo.
“Uzoefu wa hivi karibuni unaonesha dhahiri namna vijana wengi wanavyosumbuliwa na shinikizo la juu la damu na maradhi ya kisukari ambayo pia yanasababisha shinikizo la damu, “ alisema.
Alisema miongoni mwa sababu za ugonjwa wa shinikizo la damu ni pamoja na kuwa na uzito wa kupindukia na kukaa muda mrefu katika maeneo ya kazi bila kufanya mazoezi.




