Na NASRA KITANA
ULE usemi usemao ‘Upele Umepata Mkunaji’, umejidhirisha baada ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, kumteua Haji Manara, kuwa Msemaji wa timu zote za taifa.
Uteuzi wa Manara umetajwa kuwa na faida kubwa kwani timu za taifa zimepata msemaji bora ambaye atazinadi kwa nguvu kama alivyowahi kufanya kwa Simba, Yanga.
Simba na Yanga zilipokuwa zikishiriki michuano ya kimataifa, Manara alikuwa na ushawishi mkubwa wa kuinadi michezo ya timu hizo na kuzipa wasiwasi timu pinzani.
Kauli mbiu ya ‘Kwa Mkapa Hatoki Mtu’ aliyoitumia Manara akiwa Simba, iliwavutia mashabiki wengi kujitokeza dimbani kuishuhudia timu yao ikifanya nini katika mashindano ya Ligi ya Mabingwa.
Kwa kauli mbiu hiyo, Simba ilifanikiwa kwa asilimia 99 kuzifunga timu pinzani zilizotia mguu katika uwanja huo.
Manara, Diwani wa Kata ya Kariakoo, anasifika kwa kuwa na uwezo mkubwa wa kuzisemea timu za mpira wa miguu, miaka kadhaa iliyopita, kwa nyakati tofauti, alifanya kazi Simba, Yanga kama ofisa wa habari na mawasiliano kwa mafanikio makubwa.
Uteuzi wa Manara kuwa msemaji wa timu za taifa, ulitangazwa jijini Dodoma jana na Waziri wa Habari, Sanaa na Utamaduni, Paul Makonda, akiweka wazi kuwa msemaji huyo atafanya kazi chini ya Baraza la Michezo la Taifa (BMT).
Waziri huyo alisema Manara atakuwa na jukumu la kuzisemea timu zote za Taifa za mpira wa miguu na kuimarisha mawasiliano kati ya mashabiki na uongozi wa michezo nchini.
Makonda alisema uteuzi huo ni sehemu ya jitihada za kuongeza nguvu katika mawasiliano, masoko na taswira ya timu za Taifa ndani na nje ya nchi, katika kipindi hiki ambacho Tanzania inajiandaa na mashindano ya fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2027), zitakazofanyika pamoja na Kenya na Uganda.
“Manara atakuwa na kazi ya kutoa taarifa za kinachoendelea katika timu zetu zote za taifa zitakazoshiriki michuano mbalimbali, kuwanadi wachezaji, kufikisha ujumbe na ratiba zote za timu na kuchochea hamasa na kuwafanya vijana kujivunia nchi yao na vipaji,” alisema.
Aliongeza kuwa kila Mtanzania anapaswa kujua mwenendo wa timu za taifa, kupata habari ya nini timu zimefanya na malengo yake.
“Hivi sasa timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’, inafanya mazoezi, Timu ya vijana chini ya miaka 17 ‘Serengeti Boys’ na Serengeti Girls zipo katika michuano ya kimataifa lakini hakuna anayefahamu, hivyo Manara atakuwa na kazi ya kutoa habari,” alisisitiza.
UHURU lilipomuuliza Manara kuhusu uteuzi huo alisema aliishukuru serikali kwa kutambua mchango wake katika soka la Tanzania.
“Nimefanya kazi ya habari kwa miaka mingi, naijua kazi hii vilivyo na hapa ndio mahala pake, niahidi kufanya kazi kwa weledi kwa ushirikiano wa wadau wote wa michezo nchini,” alisema Manara.
Alisema anawaomba wadau wa michezo kushirikiana kwa lengo la kuweka mbele uzalendo kwa maslahi ya timu za taifa.
MAONI YA WADAU
Shabiki wa Yanga, Juma Kiyao, mwenye kadi namba 30067, alisema serikali haijakosea kumpa nafasi hiyo Manara ambaye anaijua vyema kazi hiyo.
Kiyao alisema ushaiwishi wa Manara unaweza kurudisha mioyo ya Wantanzania ambao katika siku za hivi karibuni wamepoteza mapenzi kwa timu zao za taifa.
“Miaka michache iliyopita ukisikia timu ya taifa inacheza, mashabiki tulijazana uwanjani, tuliishangilia timu bora kuchoka na huo ndio uzalendo, lakini kwa kuwa hamasa ilipotea, timu ilipoteza mvuto na wengi hatukujua kinachoendelea,” alisema.
Zuhura Majaliwa alisema ana uhakika kwa sasa atajua kila kinachoendelea katika timu za taifa kwa kuwa anajua Manara atapaza sauti.
Alisema uteuzi wa Manara utasaidia kuzinadi timu za taifa ambazo kwa sasa zinafanya vizuri katika mashindano ya kimataifa.
Alfred Samweli alisema mamlaka husika za michezo nchini zinapaswa kumpa nafasi msemaji huyo kufanya kazi yake.
Alisema kwa pamoja mashabiki wa timu za taifa wanapaswa kuzisapoti timu na kurudisha hadhi ya timu hizo kama ilivyokuwa wakati Taifa Stars ikinolewa na Mbrazili Marcio Maximo.




