RABAT, Morocco
FAINALI za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2025, zimeanza kuchezwa jana nchini Morocco.
Michuano hiyo ya 35 inashirikisha timu 24 kutoka kanda mbalimbali za bara la Afrika.
Jumla ya makundi sita yamepangwa ambapo kila kundi limehusisha timu nne.
Kundi A linaundwa na mwenyeji Morocco pamoja na timu za Mali, Zambia na Comoros wakati kundi B likiwa na Misri, Afrika Kusini, Angola pamoja na Zimbabwe huku kundi C lina timu za Tanzania ‘Taifa Stars’, Nigeria, Tunisia na Uganda.
Senegal inaunda kundi D na timu za Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Benin na Botswana wakati Algeria ipo kundi E na timu za Burkina Faso, Guinea ya Ikweta na Sudan huku kundi F likiwa na bingwa mtetezi Ivory Coast na timu za Cameroon, Gabon na Msumbiji.
Mashindano hayo yatachezwa katika viwanja tisa vilivyopo kwenye majiji sita tofauti nchini humo.
Majiji hayo ni Casablanca, Rabat, Marrakesh, Agadir, Fez na Tangier.
STADE MOHAMMED V
Uwanja wa soka wa Mohammed V utatumika katika michuano hiyo, una uwezo wa kuingiza watu 45,000.
Dimba hilo la aina yake lipo katika jiji la Casablanca.
Mji huo mkubwa zaidi katika nchi hiyo na kituo kikuu cha biashara na uchumi wa taifa hilo, unatarajiwa kuwa kivutio kikubwa zaidi kwa wageni katika michuano hiyo.

ADRAR
Uwanja huo unaoingiza mashabiki 45,000 unatarajiwa kutumika katika michuano ya AFCON mwaka huu.
Dimba hilo lililopo katika jiji la Adrar linatarajiwa kuwa kivutio kwa mashabiki wa soka kutokana na ubora wake wa muonekano.

FEZ
Katika jiji hilo lililopo Kaskazini mwa Morocco, uwanja utakaotumika katika fainali za AFCON ni Fez wenye uwezo wa kuingiza mashabiki wa soka 45,000.
Uwanja huo pia unatarajiwa kutumika kwa mechi za timu ya taifa ‘Taifa Stars’ ikiwemo dhidi ya Nigeria ambao utachezwa kesho.
MARRAKESH
Uwanja wa Marrakesh ndiyo utatumika katika fainali hizo ambao utakuwa na uwezo wa kuingiza mashabiki 45,000.
Dimba hilo lipo katika jiji la Marrakesh ambalo ni jiji la nne kwa ukubwa nchini Morocco ambapo jiji hilo lipo magharibi mwa Milima ya Atlas.

VIWANJA VINNE VYA RABAT
Rabat ndiyo mji mkuu wa Morocco na jiji la saba kwa ukubwa nchini humo.
Katika jiji hilo, kuna viwanja vinne vya soka ambavyo vitatumika katika fainali za AFCON mwaka huu.
Viwanja hivyo ni Prince Moulay Abdellah wenye uwezo wa kuingiza mashabiki 68,700, Moulay Hassan unaoingiza mashabiki 22,000, Rabat Olympic unaoingiza mashabiki 21,000 na Al Medina unaoingiza mashabiki 18,000.

TANGIER GRAND
Uwanja wa Tangier Grand utatumika katika michuano hiyo, ambapo dimba hilo lina uwezo wa kuingiza mashabiki 75,600.
Tangier ni jiji lililopo Kaskazini Magharibi mwa Morocco katika pwani ya bahari ya Mediterranean na Atlantic.




