Na AMINA KASHEBA
BONDIA wa ngumi za kulipwa, Mtanzania Fadhili Majiha, amesema anaendelea kujipanga vyema kuutetea mkanda wake wa ubingwa WBO Afrika.
Majiha atapanda ulingoni kutetea mkanda huo Januari 31 mwaka huu, jijini Dar es Salaam, ambapo hadi sasa bondia atakayechapana naye hajajulikana.
Akizungumza Dar es Salaam, Majiha alisema mashabiki na wadau wa ngumi nchini wategemee burudani bora kutoka kwake.
Alisema muda umefika wa yeye kutetea mkanda huo wenye thamani kubwa.
“Ninahitaji sapoti kutoka kwa wadau wa ngumi kwani Januari 31, mwakani, ninatarajia kutetea mkanda wa ubingwa WBO Afrika, muda umefika wa kuonyesha kazi nzuri kwa Watanzania.
“Mpinzani atawekwa wazi ni bondia mwenye viwango kutokana na aina ya mkanda ambao tunacheza, najua Watanzania na mashabiki zangu wanatambua uwezo wangu na kazi ambayo mara nyingi nimekuwa nikifanya bila ya kuwaangusha, “alisema Majiha.
Bondia huyo alisema hivi sasa anafanya mazoezi ya kujiandaa na pambano hilo kwani malengo yake ni kuendelea kumiliki mkanda huo, ndiyo maana anapambana kujiweka fiti.
Kocha wa bondia huyo, Kwame Khamisi, alisema burudani nzuri inakuja hivyo ni muhimu kumuombea dua Majiha afanye kazi yenye kiwango kikubwa.
Alisema mara nyingi Majiha anakutana na mabondia wagumu ambao Afrika wamekuwa tishio,lakini yeye anawapiga na kupata ushindi bila tatizo.




