NA MUSSA YUSUPH
NI heshima kubwa kwa Tanzania kauli ambayo imedhihirika baada ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kutunukiwa Shahada ya Udaktari wa Heshima (Honoris Causa) kutoka Chuo Kikuu cha Urafiki wa Watu cha Urusi (RUDN) ambapo amesisitiza kwamba elimu ndiyo silaha muhimu ya maendeleo duniani.
Dk. Samia alitunukiwa shahada hiyo na Mkuu wa chuo hicho, Profesa Oleg Yastrebov katika hafla iliyofanyika chuoni hapo jijini Moscow nchini Russia.
Rais Dk. Samia alitunukiwa shahada hiyo ikiwa ni kutambua mchango wake katika mageuzi ya sekta ya elimu, juhudi zake za kuimarisha diplomasia pamoja na mchango wake katika kuimarisha hadhi ya Tanzania kimataifa kupitia sekta ya utalii.
Mara baada ya kutunukiwa, Dk. Samia kupitia ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Istagram aliandika: “Ninalishukuru Baraza la Taaluma la Chuo Kikuu cha Urafiki wa Watu wa Urusi (RUDN) kwa kunitunuku Shahada ya Udaktari wa Heshima (Honoris Causa). Nimepokea heshima hii kwa unyenyekevu mkubwa kwa niaba ya Watanzania wote ambao ndiyo msingi wa mafanikio tunayojivunia na yanayoitangaza nchi yetu.
Aliongeza: “Chuo hiki ni sehemu muhimu ya maendeleo tuliyonayo kwani maarifa, ujuzi, nidhamu na weledi ambao zaidi ya Watanzania 1,100 wamepata kusoma hapa, vimechangia ustawi wa wananchi, kuijenga nchi yetu na kuimarisha uhusiano wetu. Mchango huu bado unahitajika sawa na ilivyokuwa wakati kinaanzishwa.”
ATOA MSISITIZO WA ELIMU
Katika hotuba yake aliyoitoa chuoni hapo, alisema chuo hicho kina nafasi ya kipekee katika historia ya elimu ya kimataifa kwani tangu kuanzishwa kwake mwaka 1960, kimebeba dhamira ya kuwaleta pamoja vijana kutoka nchi mbalimbali, tamaduni na historia tofauti na kuwaandaa kulitumikia taifa.
“Ninapokea shahada hii kama Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kama binti wa Afrika, kama muumini mkubwa wa elimu na kama rafiki wa chuo hiki na watu wa Urusi. Tuzo hii siyo yangu peke yangu. Ni ya wananchi wa Tanzania walioniamini na kunipa nafasi ya kuwatumikia. Ni ya walimu waliotufundisha, wazazi waliotoa sadaka kwa ajili yetu na vijana wanaotukumbusha kila siku kuwa uongozi ni huduma,” alibainisha.
Kwa Afrika, alisema historia ya chuo hicho ina umuhimu wa kipekee na Patrice Lumumba mmoja wa alama za kudumu za mapambano ya Afrika ya uhuru na heshima.
“Inatukumbusha kwamba elimu na uhuru mara nyingi huenda sambamba na kwamba vyuo vikuu vinaweza kuwa nyenzo muhimu za ukombozi wa watu, maendeleo ya kitaifa na mshikamano wa kimataifa.
“Katika muktadha huo, Shirikisho la Urusi limekuwa mshirika muhimu wa Afrika katika harakati za ukombozi na maendeleo ya kiuchumi. Kwa Tanzania, chuo hiki siyo taasisi ya mbali bali ni sehemu ya historia yetu ya ushirikiano wa muda mrefu kati ya Tanzania na Urusi,” alibainisha.
Dk. Samia alisema ushirikiano huo katika elimu umeendelea kukua kwa miaka mingi kwani zaidi ya Watanzania 5,000 wamesoma katika Umoja wa Kisovieti na baadaye Shirikisho la Urusi.
Alisema Watanzania hao wamerudi nchini kama madaktari, wahandisi, wanasayansi, wanadiplomasia, walimu, wasimamizi na watumishi wa umma.
“Huu ndio uwezo mkubwa wa elimu. Mwanafunzi huondoka nyumbani akiwa na ndoto, huvuka mipaka kutafuta maarifa na kurudi akiwa na nyenzo za kujenga taifa lake. Katika safari hiyo, maisha ya mtu mmoja hubadilika, familia hubadilika, jamii hubadilika na hatimaye taifa zima hubadilika.
Alisisitiza: “Wakati Tanzania ilipopata uhuru, fursa za elimu zilikuwa chache sana. Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kilipoanzishwa mwaka 1961 kilianza na wanafunzi wasiofika 20. Leo, Tanzania ina vyuo vikuu na vyuo vikuu shiriki 52 vya umma na binafsi, vyenye zaidi ya wanafunzi 250,000 wanaojiunga kila mwaka.”
AZUNGUMZIA UMUHIMU WA SAYANSI
Katika hotuba yake, Dk. Samia alisema dunia inabadilika kwa kasi kupitia teknolojia za kidijitali, akili Unde (AI), sayansi ya data, bioteknolojia na tiba za kisasa, hivyo Tanzania na Afrika kwa ujumla haziwezi kubaki nyuma.
“Ndiyo maana Dira ya Maendeleo ya Tanzania 2050 inaweka maarifa, ujuzi, sayansi, teknolojia na ubunifu katika kiini cha ajenda ya mabadiliko ya Taifa. Tunafahamu kuwa miundombinu ni muhimu, lakini tunajua pia kuwa na miundombinu peke yake haiwezi kubadilisha taifa. Mabadiliko yanahitaji watu wenye ujuzi, wabunifu, wazalendo na wanaotumia maarifa kwa manufaa ya wote.
“Katika muktadha huo, Chuo Kikuu cha Urafiki wa Watu cha Urusi kinaendelea kuiunga mkono Tanzania kwa kuwaandaa vijana wetu kuwa tayari kulitumikia taifa lao,” alibainisha.
Alisema mwaka 2023 serikali ilianzisha Mpango wa ‘Samia Scholarship’ ili kuwasaidia wanafunzi bora wa Kitanzania hususan katika masomo ya sayansi, teknolojia, uhandisi, hisabati, tiba na maeneo mengine ya kimkakati.
Alibainisha kuwa lengo ni kuhakikisha hakuna mwanafunzi mwenye uwezo wa kitaaluma anayekosa elimu bora kwa sababu ya changamoto za kifedha.
“Mpango huo hadi sasa umewasaidia zaidi ya wanafunzi 5,000 katika taaluma za STEM. Tunaendelea kupanua fursa kwa wanafunzi kufanya masomo ya juu katika sayansi ya data, Akili Unde, tiba, uhandisi, mafuta na gesi, sayansi ya mazingira na teknolojia zinazohusu mabadiliko ya tabianchi.
“Huu siyo mpango wa elimu tu, ni uwekezaji wa taifa katika siku zijazo. Ni uwekezaji kwa daktari atakayeokoa maisha, mhandisi atakayejenga miundombinu, mwanasayansi atakayesuluhisha changamoto, mbunifu atakayezalisha ajira na mwalimu atakayelea vizazi vijavyo.
Alisisitiza: “Ninaona fursa kubwa ya kuimarisha ushirikiano kati ya vyuo vikuu vya Tanzania na Chuo Kikuu cha Urafiki wa Watu wa Urusi kupitia ufadhili wa masomo, tafiti, kubadilishana wanafunzi na wahadhiri pamoja na kuendeleza mitaala inayolingana na vipaumbele vya maendeleo ya Tanzania.”




