Na VICTOR MKUMBO
UKARABATI wa Uwanja wa Benjamin Mkapa, jijini Dar es Salaam umefikia asilimia 90% kukamilika hivi sasa.
Kwa mujibu wa Mratibu wa Viwanja nchini, Milinde Mahona ukarabati wa Uwanja wa Benjamin Mkapa, umefikia asilimia 90 kukamilika.
Alisema hivi sasa zimebakia asilimia 10 kuhakikisha uwanja huo unakamilika na ambapo unatarajiwa kutumika katika michuano mbalimbali ikiwemo Kombe la Mataifa Afrika (AFCON 2027).
“Hivi sasa Uwanja wa Benjamin Mkapa tayari umeshakamilka kwa asilimia 90 na kwamba zimebakia asilimia 10.
“Ukarabati unakwenda vizuri tuna imani utakamilika kwa wakati kwani ni moja ya viwanja vitakavyotumika katika michuano ya AFCON 2027 ambapo Tanzania tutakuwa wenyeji kwa ushirikiano wa nchi za Kenya na Uganda,” alisema Mahona.
Alisema ukarabati wa uwanja huo umefanyika katika maeneo mbalimbali yakiwemo uwanja (pitch), kufunga viti vipya, kufunga taa ndani na nje na sehemu ya kukaa waandishi wa habari.
Alisisitiza kwa upande wa ujenzi wa Uwanja wa kisasa wa mpira wa soka Arusha, hivi sasa unandelea kufanyika kwa kasi ambapo umefikia asilimia 66.
Alisema awali Oktoba, mwaka huu ujenzi wa uwanja huo ulikuwa umefikia asilimia 63.5.
Uwanja huo ambao upo katika eneo la Olomoti, Arusha ukikamilika unatarajiwa kuwa na uwezo wa kuchukua watazamaji 30,000.
“Ujenzi wa Uwanja Arusha unaendelea kwa kasi ambapo hivi sasa umefikia asilimia 66.
Alisema uwanja huo utamilika kwa wakati kuhakikisha unatumika katika fainali za michuano AFCON 2027 na mashindano mbalimbali.
“Mafundi wanaendelea kufanya kazi kwa kasi na hivi sasa ujenzi wa uwanja wa Arusha umeshafikia asilimia 66.
“Hivi sasa mafundi wameshaanza kuchimba eneo la kuchezea mpira ‘pich’ huku maeneo mengine yakiwa tayari yamekamilika yakiwemo majukwaa ya watazamaji.
“Mbali ya kuanza kuchimba eneo la kuchezea, maeneo mengine ambayo yanafanyiwa kazi kwa ubunifu ni paa la uwanjani, ufungaji wa miundombinu ya umeme, zimamoto, TEHAMA na kuweka mabomba,” alisema.
Mratibu Mahona, alisema kukamilika kwa uwanja huo utalenga kuongeza miundombinu ya michezo nchini na kupanda kwa hadhi kutokana na ubora wake.
“Pia mafundi wanaendelea kufanya kazi kwa bidii huku nje ya uwanja ujenzi ukiendelea ikiwemo maeneo ya kuegeshea magari,” alisema.
Aliongeza kwa upande wa Uwanja wa soka wa Dodoma, hivi sasa wameshaanza kusafisha eneo na baadaye ujenzi utaanza mara moja.
Ujenzi wa Uwanja wa Arusha, Dodoma na ukarabati wa Benjamin Mkapa na Uhuru ni juhudi za Serikali chini ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kuhakikisha michezo inafanyika katika miundombinu bora zaidi.




