Na MWANDISHI MAALUMU
MJUMBE Maalumu wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN), Parfait Onanga-Anyanga, amesema umoja huo unatambua na kupongeza hatua zinazochukuliwa na Serikali ya Tanzania, baada ya matukio ya Oktoba 29, mwaka jana.
Pia, umepongeza uamuzi wa kuunda Tume Huru ya Uchunguzi na dhamira ya kufanya mazungumzo jumuishi ya kitaifa pamoja kuendeleza mchakato wa mabadiliko ya kikatiba.
Onanga-Anyanga aliyasema hayo, alipokutana na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, alipowasilisha salamu za Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres, Ikulu Chamwino, mkoani Dodoma.
Mjumbe huyo, yuko nchini kusikiliza maoni ya wadau na kutathmini hatua zinazochukuliwa na serikali katika kuimarisha utulivu wa kisiasa, mshikamano wa kitaifa na kuendeleza misingi ya utawala wa sheria kufuatia matukio ya uvunjifu wa amani ya kabla na wakati wa uchaguzi mkuu Oktoba 29, mwaka jana.
Katika mazungumzo yao, mjumbe huyo alisema umoja huo unaendelea kuitambua Tanzania kama nchi yenye historia ya muda mrefu ya amani, utulivu wa kisiasa na mshikamano wa kitaifa, pamoja na kuthamini mchango wake katika juhudi za kulinda na kuimarisha amani barani Afrika.
Katika ziara yake, Onanga-Anyanga alikutana na kuzungumza na viongozi wa taasisi mbalimbali nchini, ikiwemo Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mahakama ya Tanzania, Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa pamoja viongozi wa vyama vya siasa.
Aidha, alikutana na kufanya mazungumzo na Mwenyekiti na wajumbe wa Tume Huru ya Uchunguzi pamoja wadau wengine wa kisiasa na kijamii kupata maoni na mitazamo tofauti kuhusu masuala yaliyotokea na hatua zinazoendelea kuchukuliwa na serikali.
Onanga-Anyanga alisema ushirikiano huo utawezesha umoja huo kupata taswira halisi kuhusu uhalisia wa matukio ya Oktoba 29, mwaka jana na jitihada zinazofanywa na Serikali ya Tanzania katika utatuzi wa changamoto zilizojitokeza wakati na baada ya matukio hayo.
Kwa mujibu wa Onanga-Anyanga, hatua hizo zina mchango muhimu katika kuimarisha maridhiano ya kitaifa, kurejesha imani ya wananchi na kuendelea kujenga taasisi imara za kidemokrasia nchini.
Mjumbe huyo aliahidi kuwasilisha tathmini ya mashauriano hayo kwa Katibu Mkuu wa umoja huo, kuendelea kuyaimarisha kati ya Umoja wa Mataifa na Tanzania.
RAIS DK. SAMIA
Kwa upande wake, Rais Dk. Samia alituma salamu za shukrani na kupongeza hatua ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Guterres ya kutuma ujumbe maalumu nchini Tanzania kupata uelewa wa kina kuhusu hali ya nchi na kusikiliza maoni ya wadau mbalimbali.
Rais Dk. Samia alisema Serikali ya Tanzania imejizatiti kuhakikisha mchakato wa kufuatilia matukio hayo unafanyika kwa kuzingatia misingi ya utawala wa sheria, uwajibikaji na haki, ikiendelea kulinda amani, umoja wa kitaifa na utulivu wa kisiasa ambao umekuwa msingi wa maendeleo ya nchi.
Alieleza kuwa serikali iko tayari kupokea na kuyafanyia kazi mapendekezo yatakayowasilishwa na Tume ya Uchunguzi mara baada ya kukamilika kwa kazi yake, mapendekezo hayo yatakuwa sehemu muhimu ya mchakato wa kuimarisha maridhiano ya kitaifa, pamoja na marekebisho ya Katiba.
Vilevile, Rais Dk. Samia alisisitiza kwamba Tanzania itaendelea kushirikiana na Umoja wa Mataifa na Jumuiya za Kimataifa katika kukuza demokrasia, utawala bora na maendeleo jumuishi.




